Ligi Kuu ya NBC inaendelea leo ambapo mechi mbili zinatarajiwa kupigwa jijini Dar es salaam na kule visiwani Zanzibar
Yanga itakuwa mwenyeji wa Azam Fc katika Derby ya Dar es salaam, mchezo ukitarajiwa kupigwa uwanja wa Azam Complex saa 12 jioni na kufuatiwa na mchezo kati ya Singida Black Stars dhidi ya Coastal Union utakaopigwa uwanja wa New Amaan Complex, saa 2:30 usiku
Macho na masikio ya mashabiki wengi wa soka yameelekezwa kule Azam Complex ambao mchezo kati ya Yanga dhidi ya Azam Fc utapigwa
Yanga na Azam Fc zimetoa mechi bora yenye ushindani katika misimu ya karibuni. Wengi wanaamini ukitoa derby ya watani wa jadi, Derby ya Dar kati ya Yanga na Azam Fc ni mchezo wa pili wenye mvuto zaidi
Wakiwa kileleni mwa msimamo wa ligi, Yanga wataingia katika mchezo huo wakizisaka alama tatu ili waendelee kutimua vumbi pale juu
Hata hivyo haitakuwa kazi rahisi mbele ya Azam Fc, timu pekee iliyoifunga Yanga kwenye ligi mwaka 2023
Ndio! March 17 2023 Azam Fc iliichapa Yanga mabao 2-1 katika mchezo wa ligi kuu uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa
Tangu wakati huo, Yanga haijapoteza mchezo wowote ndani ya ligi kuu wakicheza mechi 17, kushinda mechi 16 na kutoka droo mechi moja
Ushindi au hata sare kwa Azam Fc mbele ya Yanga leo utaweka rekodi nyingine kwa matajiri hao wa Chamazi pengine kuwa timu ya kwanza kuizuia Yanga msimu huu
Ikumbukwe msimu huu Yanga imeshinda mechi zote nane, ikifunga mabao 13 pasipo kuruhusu bao upande wao
Ni wazi Azam Fc watahitaji kuwa kwenye ubora wao, kuizuia Yanga ambayo mapema msimu huu ilibeba Ngao ya Jamii kwa ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Azam Fc




