Mlinda lango wa Simba Aishi Manula amesema licha ya kutopata nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza, anashirikiana vyema na wenzake katika kuhakikisha timu inafikia malengo ya kutwaa ubingwa wa ligi kuu msimu huu
Jana Manula aliiongoza timu ya Taifa ya Tanzania 'Taifa Stars' kwa wachezaji wa ndani katika mechi ya kuwania kufuzu fainali za CHAN 2025 Tanzania ikipoteza kwa mikwaju ya penati 6-5 baada ya sare ya bao 1-1 (aggregate)
Manula amesema anafuraha kuwa sehemu ya kikosi cha Simba msimu huu licha ya kutoonekana mara kwa mara uwanjani
"Nimekuwa nikifanya mazoezi ndani ya Simba chini ya makocha bora, hivyo hata kama sichezi nimekuwa katika ubora na utimamu mzuri ndio maana nimepata nafasi kuitumikia timu ya Taifa"
"Ninashirikiana vyema na wenzangu hata kama sionekani uwanjani nikicheza, kama timu tuna lengo moja, haijalishi nani anaanza lakini dhamira yetu ni kuona tunatimiza lengo la kutwaa ubingwa"
"Nafurahi nimepata nafasi ya kuonyesha nilichonacho timu ya Taifa, nitaendelea kupambana kwani naamini wakati utafika nitacheza," alisema Manula
Msimu huu Manula alipata nafasi ya kuichezea Simba katika mechi moja ya kirafiki dhidi ya Al Hilal iliyomalizika kwa matokeo ya sare ya bao 1-1
Imekuwa si rahisi kwake kupenya katika kikosi cha kwanza mbele ya Moussa Camara, Ali Salim na hata Ayoub Lakred ambaye amerejea hivi karibuni baada ya kuwa nje kwa miezi kadhaa akiuguza majeraha



