Kocha Mkuu wa Singida Black Stars, Patrick Aussems, amesema kikosi chake kitafanya 'maajabu' msimu huu kutokana na aina ya wachezaji alionao
Aussems amesema anaiona timu yake ikifanya vizuri msimu huu na kutoa ushindani kwa klabu kubwa hapa nchini katika mechi za Ligi Kuu Tanzania Bara inayoendelea
"Nimekuwa hapa Tanzania kwa miaka kadhaa, naifahamu Ligi Kuu, najua timu kubwa zilizozoeleka ni Simba, Yanga na Azam lakini naiona timu yangu ikiwa kwenye mwelekeo mzuri, tunaweza tukafanya kitu ambacho wengi hawategemei," alisema Aussems
Alisema kikosi chake kina wachezaji wenye uwezo mkubwa, wanaojituma na wanauwezo wa kuipa timu hiyo matokeo mazuri katika mechi zao zijazo
Aliongeza lengo lake ni kuona timu inaendelea kufanya vizuri na kumaliza katika nafasi za juu ili kupata tiketi ya kushiriki mashindano ya kimataifa mwakani
"Hili linawezekana kama tutaendelea kufanya kazi nzuri, wachezaji kujituma na uongozi kufanya kazi yao, hakuna kisichowezekana, naamini tutafanya vizuri," Aussems aliongeza
Singida Black Stars wako katika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi wakikusanya alama 23 kutoka mechi 10. Wamezidiwa alama moja tu na Yanga inayoshika nafasi ya pili ikiwa na alama 24 huku Simba ikiwa kileleni na alama 25
Hata hivyo Yanga ina mchezo mmoja wa kiporo ambapo leo Alhamisi itacheza dhidi ya Tabora United



