Kiungo wa Singida Black Stars, Marouf Tchakei, amesema tuzo ya mchezaji bora wa mwezi Oktoba ni chachu kwake ya kuendelea kufanya vizuri kwenye kikosi cha timu yake
Nyota huyo raia wa Togo wiki iliyopita alitangazwa kuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu kwa mwezi Oktoba pamoja na kocha wa Azam FC, Rachid Toussi aliyetangazwa kuwa kocha bora
Tchakei amebainisha kuwa tuzo hiyo imempa hamasa ya kuendelea kujituma kwenye timu yake na kusaidia kufanya vizuri
"Nawashukuru wachezaji wenzangu kwa ushirikiano wao, hii tuzo ni chachu ya kuendelea kufanya vizuri na kusaidia timu kufanya vizuri zaidi," alisema nyota huyo
Alisema ligi ni ngumu na yenye ushindani hivyo lazima kama wachezaji wajitume katika kila mchezo kuweza kupata ushindi utakaoisaidia timu hiyo kuendelea kukaa kwenye nafasi za juu
Singida Black Stars inashika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 23 baada ya kucheza michezo 10 ikizidiwa kwa pointi mbili na vinara wa Ligi hiyo, Simba huku Yanga ikiwa kwenye nafasi ya pili na pointi 24



