Mchezo wa ligi kuu kati ya Tabora United dhidi ya Singida Black Stars uliopigwa uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mkoani Tabora asubuhi ya leo, Jumatatu Novemba 25, umemalizika kwa matokeo ya sare ya mabao 2-2
Mchezo huo ambao ulipaswa kupigwa jana, uliahirishwa baada ya mvua kubwa kunyesha mkoani Tabora na kujaza maji uwanja wa Ali Hassan Mwinyi
Singida Black Stars watajilaumu wenyewe kwa kushindwa kuondoka na alama zote tatu, wakipoteza uongozi wa mabao mawili waliyofunga katika kipindi cha kwanza
Elvis Rupia alitangulia kufunga bao la uongozi kwenye dakika ya 16 kabla ya Anthony Trabi kuongeza bao la pili katika dakika ya 32
Hata hivyo Yacouba Songhne alipunguza mzigo kwa Tabora United kabla ya mapumziko akifunga bao mahiri baada ya kuwazidi ujanja walinzi wa Singida BS pamoja na mlinda lango wao Metacha Mnata
Heritier Makambo aliweka mzani sawa dakika nne baada ya kuanza kipindi cha pili akimalizia kazi nzuri iliyofanywa na Yacouba aliyeonyesha kiwango bora katika mchezo huo
Matokeo hayo yanaibakisha Singida BS katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi wakiwa na alama 24 sawa na Azam Fc na Yanga ambazo zina uwiano mzuri zaidi wa mabao
Tabora United imesogea hadi nafasi ya tano katika msimamo baada ya kufikisha alama 18



