Aliyekuwa kocha wa Singida Black Stars Patrick Aussems amewaaga wanafamilia wa timu hiyo baada ya mkataba wake pamoja na kocha msaidizi kusitishwa ghafla wiki iliyopita
Katika salamu zake za shukrani, Aussems amewashushia lawama viongozi wa Singida BS kuwa wamekosa weledi wa kuiendesha tmu hiyo
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Aussems ameandika ujumbe huu;
"Hakika maamuzi yaliyofanyika hayakua kwa sababu ya matokeo. Ilikua furaha kufundisha kundi hili la wachezaji. Lakini Ilikua ni kama jinamizi kila siku kufanya kazi na uongozi usiokua na weledi"
"Nilikua nikilalamikia kila siku kuhusu kukosekana kwa uwezo katika uongozi. Msaidizi wangu, Denis Kitambi na mimi binafsi hatujashangazwa na maamuzi yaliyofikiwa, ilikua ni kama ahueni kwetu"
"Hivyo nadhani sasa mmeshaelewa tatizo lilikua wapi. Ningependa kuwashukuru maelfu ya watu kila kona ya nchi kwa miezi mitano iliyopita waliokuja kwangu kunitakia heri, na kupiga na mimi selfie"
"Najiona bado nilikua napendwa sana na mashabiki wa Simba pamoja na watu wengine pia. Nathamini sana wema na ukarimu wenu. Mwisho, kama isemavyo methali ya kifaransa 'Jamais 2, Sans 3'. Kwa maana ya kuwa jambo ambalo limeshatokea mara mbili nyuma upo uwezekano litatokea mara ya tatu siku za mbeleni. Hivyo labda inawezekana tutaonana tena hivi karibuni," aliandika Aussems



