Baada ya kikosi kutua salama Algiers jana, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe amesema hawana wasiwasi wowote kuelekea mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya wenyeji MC Alger utakaochezwa Jumamosi uwanja wa July 05 1962
Yanga itashuka katika mechi hiyo ya pili ya hatua ya makundi ikiwa na kumbukumbu ya kufungwa mabao 2-0 na Al Hilal ya Sudan, mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam wiki iliyopita
Kamwe amesema kikosi kimewasili salama na kila mchezaji yuko katika hali nzuri kwa ajili ya kuipambania timu
Kamwe amebainisha kuwa watakuwa na takribani siku mbili za maandalizi wakiwa Argeria chini ya benchi la ufundi linaloongozwa na Kocha Mkuu, Sead Ramovic
"Tunashukuru timu imewasili salama hapa Algiers, tulipata changamoto kidogo ya kuchelewa kutoka uwanja wa ndege baada ya kutua kutokana na taratibu za Kimataifa lakini kila kitu sasa kinakwenda vizuri," alisema Kamwe
Mechi dhidi ya MC Alger itachezwa kwenye Uwanja wa Julai 5, 1962 baada ya maombi ya kuhamishiwa kwenye Uwanja wa Ali la Pointe kukataliwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF)
MC Algers ilitaka kupeleka mchezo huo katika Mji wa Douera uliopo kilomita 19 kutoka jijini Algers. Taarifa kutoka CAF zimethibitisha mchezo huo utachezwa kwenye uwanja uliopangwa na kupitishwa na CAF awali
CAF imewafungia MC Algers kucheza michezo minne bila mashabiki kutokana na makosa ya utovu wa nidhamu yaliyoonyeshwa na mashabiki wao katika mechi ya mwisho ya kufuzu hatua hiyo ya makundi waliyocheza dhidi ya US Monastir ya Tunisia



