Ramovic anataka ushindi Algeria

Joel JJ By Joel JJ β€’ 6th December 2024


Ramovic anataka ushindi Algeria

Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya MC Alger ambao utapigwa kesho Jumamosi katika uwanja wa July 05 1962

Akizungumza katika mkutano na wanahabari, Ramovic amesema anatambua mchezo huo utakuwa mgumu kwani wanakwenda kucheza dhidi ya timu ngumu lakini anaamini katika ubora wa timu yake na ana imani watafanya vizuri katika mchezo huo

Ramovic amesema Yanga ina historia katika uwanja wa July 05, hivyo kesho itakuwa siku nyingine kwao kusaka ushindi

"Tunakwenda kucheza na timu ngumu, ina wachezaji bora na kocha mzoefu lakini upande wetu tuna kikosi chenye wachezaji bora sana, naamini itakuwa mechi nzuri yenye kuvutia"

"Yanga wana historia kwenye uwanja tutakaotumia kesho, walipoteza mchezo wa Fainali hapa kwa kanuni lakini naamini walishinda mioyo ya wapenda mpira hapa Algeria, kesho ni siku nyingine na tutakuja na nguvu nyingine ya kutaka kushinda mchezo," alisema Ramovic

Kocha huyo raia wa Ujerumani ameongeza kuwa kupoteza mchezo wa kwanza dhidi ya Al Hilal kumewaongezea morali katika maandalizi ya mchezo wa kesho ambao wanahitaji kushinda

"Tuko kwenye presha baada ya kupoteza mchezo wa kwanza, lakini imetupa nguvu ya kujiandaa vizuri kuelekea mchezo wa kesho"

"Tumekuja mapema kwa ajili ya kuzoea hali ya hewa. Hatuwezi kupanga matokeo ya mwisho yatakavyokuwa Lakini tunaweza kupanga jinsi tutakavyocheza ili kupata matokeo mazuri"

"Sio nzuri kucheza mechi bila mashabiki, binafsi napenda kuiona timu yangu ikicheza mbele ya mashabiki wengi, lakini kwa kesho tutawakosa mashabiki hapa uwanjani hivyo tuna jukumu la kupambana kuwapa furaha mashabiki wetu watakaokuwa nyumbani," alisema

Akizungumza kwa niaba ya wachezaji wenzake, Stephane Aziz Ki amesema wamejifunza kutoka kile kilichotokea katika mechi mbili zilizopita, kesho wanakwenda kupambana kusahihisha makosa

"Kila siku mpya uwanjani inatupa nafasi wachezaji ya kujifunza kitu kipya, mechi mbili zilizopita, ya Ligi ya Mabingwa na Ligi Kuu zimetupa funzo na kesho tutakwenda kupambana ili tupate matokeo mazuri," alisema Aziz Ki


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.