Wakati zimebaki siku sita tu kabla ya dirisha dogo la usajili kufunguliwa, Klabu ya Yanga ipo kwenye hatua za mwisho kupata saini ya kiungo mkabaji wa Singida Black Stars, Kelvin Nashon, imefahamika
Habari kutoka ndani ya Yanga, zinasema kuwa mchezaji huyo ana asilimia kubwa ya kujiunga na Yanga kwa mkataba wa mkopo wa miezi sita
Nashon anatarajiwa kutua kuongeza nguvu kusaidiana na Khalid Aucho ambaye kwa sasa amekuwa akiandamwa na majeraha ya mara kwa mara, akicheza pia mechi nyingi ambazo zimeonekana kuathiri kiwango chake
"Nadhani Nashon anaweza kutusaidia kwa sasa, tutamchukua kwa mkataba wa muda mfupi wa miezi sita, kama akifanya vizuri, basi mwishoni mwa msimu tutakaa na Singida Black Stars kwa ajili ya kufanya biashara nyingine, kwani tutamsajili kwa miaka miwili"
"Angalia hivi sasa kocha wetu, Sead Ramovic, ameamua kumchezesha Duke Abuya namba sita, wakati ni winga na kiungo mshambuliaji, kwa sababu tuna mapungufu kidogo kwenye eneo hilo, tunachohitaji ni ubora na Nashon timu zote alizoenda ameonekana yupo imara na kiwango chake hakishuki," alisema mtoa taarifa



