Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ali ametangaza viingilio vya mchezo wa tatu wa hatua ya makundi kombe la Shirikisho (CAF CC) dhidi ya CS Sfaxien ambao utapigwa Jumapili, Disemba 15 katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Ili kuhakikisha Wanasimba wengi wanajitokeza uwanja wa Benjamin Mkapa kuishangilia timu yao, Ahmed amesema uongozi umepunguza bei ya viingilio ambapo majukwaa pendwa ya Mzunguuko kiingilio ni Tsh 3,000/-
- Tanzanite - Tsh. 250,000
- Platinum - Tsh. 150,000
- VIP A - Tsh. 30,000
- VIP B - Tsh. 20,000
- VIP C - Tsh. 10,000
- Machungwa - Tsh. 5,000
- Mzunguko - Tsh. 3,000
Aidha Ahmed amesema lengo ni kuhakikisha wanakwenda kujaza uwanja wa Benjamin Mkapa na kuipa hamasa Simba katika mchezo ambao alama tatu lazima zbaki nyumbani
"Tarehe 15 siku ya Jumapili saa 10:00 jioni kunako Uwanja wa Mkapa ni siku ya kumuangamiza CS Sfaxien. Na hili halitawezekana kwa Fadlu peke yake, kwa Camara peke yake bali kwa Wanasimba wote kuja uwanjani, hakuna Mwanasimba anayetakiwa kubaki nyumbani. Kama kweli tuna nia ya kumuangamiza mpinzani wetu basi hatuna budi aache nyumba yake aje Benjamin Mkapa."
"Kila kiongozi wa tawi, kila kiongozi wa kundi ana jukumu la kuhimiza Wanasimba wenzake kuja uwanjani. Hakuna sababu yoyote ya Mwanasimba kubaki nyumbani. Utaipendaje Simba kama huifati ilipo?"
"Kupoteza na CS Constantine kusitutoe kwenye reli, nafasi yetu ya kwenda robo fainali bado nyeupe kabisa. Nafasi yetu bado iko wazi tukifanya vizuri mechi inayofata."
"Baada ya kupoteza mchezo wa juzi kuna wenzetu wakaanza kukata tamaa lakini niwambie tu tuko salama sana, hakuna kilichobadilika, nafasi yetu ya kwenda robo fainali iko palepale. Niwakumbushe msimu juzi mpaka mchezo wa pili hatukuwa na alama yoyote na tukaibukia kwa Vipers na kila mmoja anakumbuka Mnyama akavuka kwenda robo fainali."
"Mchezo wa Jumapili lazima kila Mwanasimba ajue umuhimu wake maana mpinzani tunayekutana nae anataka kufufukia kwetu na sisi hatuko tayari kuona CS Sfaxien anafufukia kwetu. Hakuna ambaye amewahi kupata uhai ndani ya Uwanja wa Benjamin Mkapa."
"Kwa kuwa mechi hii tunataka tuwe na mashabiki wengi Benjamin Mkapa, tunataka kujaza Benjamin Mkapa. Mara ya mwisho kujaza Uwanja wa Mkapa ilikuwa ni Simba Day. Tumeamua kuweka viingilio ambavyo havitampa mtu sababu ya kutokuja uwanjani lakini pia tupo karibu na sikukuu za mwaka. Na sisi tumeamua kupunguza viingilio ili kila Mwanasimba aje uwanjani," alisema Ahmed