Siku tano kabla ya dirisha dogo la usajili kufunguliwa, Yanga imeanza kutambulisha silaha zake mpya baada ya mabingwa hao wa Tanzania Bara kutambulisha usajili wa mlinzi wa pembeni Israel Mwenda
Mwenda ametua Yanga kwa mkopo wa hadi mwishoni mwa msimu akitokea klabu ya Singida Black Stars
Beki huyo mwenye umri wa miaka 24, anamudu kucheza nafasi zote za ulinzi wa pembeni kulia na kushoto
Kabla ya kusajiliwa na Singida Black Stars mwanzoni mwa msimu huu, Mwenda alizitumikia klabu za KMC na Simba mara kadhaa akipata nafasi ya kuitwa timu ya Taifa
Yanga inakabiliwa na changamoto katika safu ya ulinzi hasa upande wa kushoto ambapo beki tegemeo Chadrack Boka anakabiliwa na majeraha ya mara kwa mara
Mbadala wake Nickson Kibabage hajaonyesha ushawishi wa kutosha kuaminiwa katika nafasi hiyo huku Kibwana Shomari akikosekana kwenye kikosi cha kwanza kwa muda mrefu kwa kilichoelezwa kupungua makali yake



