Kocha Mkuu wa Simba Fadlu Davids amesema licha ya ugumu wa ratiba inayowakabili mbele yao, kikosi chake kiko tayari kuwania alama tatu katika mchezo unaofuata ligi kuu ya NBC dhidi ya KenGold
Baada ya mchezo wa kombe la Shirikisho dhidi ya CS Sfaxien ambao Simba iliibuka na ushindi wa mabao 2-1, kesho tena Simba inashuka dimba la KMC Complex kuikabili KenGold
Fadlu amesema baada ya kuwapa mapumziko wachezaji wake hapo jana, leo watakamilisha maandalizi kuelekea mchezo huo ambao wanazihitaji alama zote tatu
Fadlu amesema hawapaswi kuwadharau wapinzani wao licha ya nafasi waliyopo katika msimamo wa ligi kwani hawana cha kupoteza
"Tunakabiliwa naa ratiba ya kucheza mechi nne ndani ya muda mfupi lakini lazima tuwe tayari kwa ratiba hii"
"Baada ya mchezo dhidi ya CS Sfaxien, leo tutafanya maandalizi yetu ya mwisho kwa kuzingatia aina ya mpinzani tunayekwenda kucheza nae"
"Tunajua ubora wa KenGold, tunapaswa kucheza kwa tahadhari bila kuwapa nafasi ya kutushambulia kwa kushitukiza"
"Haitakuwa mechi nyepesi hivyo hatupaswi kufikiria tutakwenda uwanjani na kuchukua alama tatu tu, tutahitaji kupambana na muhimu zaidi ni kushinda mchezo huo", alisema Fadlu
Katika kipindi cha siku 10 Simba inatarajiwa kucheza mechi nne za ligi kuu. Mchezo utakaofuata baada ya KenGold ni dhidi ya Kagera Sugar utakaopigwa Disemba 21 uwanja wa Kaitaba, Kagera
Baada ya mchezo huo, Simba itarejea Dar kumenyana na JKT Tanzania Disemba 24 kisha kusafiri mkoani Singida kuikabili Singida BS, Disemba 28



