Simba yapania ushindi Angola

Joel JJ By Joel JJ β€’ 11th January 2025


Simba yapania ushindi Angola

Jana Simba ilifanya mazoezi katika uwanja wa Novemba 11 huko Angola kuelekea mchezo wa kombe la Shirikisho dhidi ya Bravos utakaopigwa kesho Jumapili, Januari 12

Simba iililazimika kujifua katika uwanja huo jana badala ya siku ya leo kulingana na kanuni zinavyoelekeza kwa kuwa leo kutakuwa na mchezo wa ligi ya mabingwa kati ya Sagrada Esperance dhidi ya Pyramids

Kikosi cha kocha Fadlu Davids kitahitimisha maandalizi yake leo tayari kwa mchezo huo utakaopigwa saa 1 usiku kwa saa za Tanzania

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba Ahmed Ali amesema maandalizi na taratibu zote kuelekea mchezo huo zimekamilika kwa upande wao

Ahmed amesema wanauchukulia mchezo huo kwa umuhimu mkubwa kwa sababu ni mchezo ambao utakwenda kuwahakikishia kufuzu robo fainali leo

"Tumefanya mazoezi katika uwanja wa Novemba 11 leo (jana) kwa kuzingatia maelekezo ya CAF kwa kuwa kesho (leo) kuna mchezo wa ligi ya mabingwa utachezwa katika uwanja huu"

"Hatuna hofu yoyote kucheza hapa, kwani haitakuwa mara ya kwanza kupata ushindi katika uwanja huu"

"Mwaka 2021 tulicheza dhidi ya timu kubwa zaidi hapa Angola Prmeiro De Agosto na kupata ushindi wa mabao 3-1"

"Tunafahamu mechi ya Jumapili itakuwa ngumu kwa sababu ni mechi ya kuamua hatma ya kufuzu robo fainali kwetu na hata kwa wapinzani wetu"

"Tuko makini, uongozi umechukua tahadhari zote na niseme tu, ari na morali ya wachezaji iko juu tukihitaji kushinda mchezo huu," alisema Ahmed

KImahesabu Simba inahitaji alama moja tu katika mchezo wa kesho ili kutinga robo fainali


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.