Simba yaingia kambini kuiwinda CS Constantine

Joel JJ By Joel JJ β€’ 15th January 2025


Simba yaingia kambini kuiwinda CS Constantine

Klabu ya Simba leo imeingia kambini kwa ajili ya maandalizi ya mchezo wa kuhitimisha hatua ya makundi kombe la Shirikisho (CAF CC) dhidi ya CS Constantine ambao utapigwa Jumapili Januari 19 katika uwanja wa Benjamin Mkapa

Akizungumza katika Mkutano na wanahabari mapema leo, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba Ahmed Ali alisema wamepania kushinda mchezo dhidi ya CS Constantine ili kumaliza kinara wa kundi A

Ahmed ametamba kuwa Simba ndio klabu kubwa katika kundi A hivyo wana kila sababu ya kuonyesha ukubwa wao siku ya Jumapili kwa kuifunga CS Constantine na kuongoza kundi A

"Leo Jumatano wachezaji wameingia kambini na kuanza mazoezi kujiandaa na mchezo wa Jumapili. Sisi Simba tunaungalia mchezo dhidi ya CS Constantine kwa ukubwa"

"Wakati makundi yanapangwa Simba ndio tuliokuwa timu kubwa kwenye kundi hivyo katika kukamilisha hatua ya makundi ni lazima kuonyesha ukubwa wetu kwa kumaliza wa kwanza. Lakini ukimaliza wa kwanza kwenye kundi, hatua ya robo unaanzia ugenini na mwisho unamalizia nyumbani."

"Tukimaliza wa kwanza na robo kuanzia ugenini, tukimalizia nyumbani tutakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuingia nusu fainali. Kwenye kundi tumezifunga timu mbili na alikuwa bado huyu wa Jumapili hivyo na yeye anatakiwa apate pumzi ya moto"

"Wapinzani wetu CS Constantine wako njiani kuja Tanzania na maafisa wetu wa Simba wako uwanja wa ndege kuwapokea," alisema Ahmed

Ahmed amekiri Simba kupata pigo baada ya CAF kuwazuia mshabiki wao kushuhudia mchezo huo

"Kuelekea mchezo wa Jumapili, Simba tumepata pigo la kubwa na pigo lenyewe ni kuzuiliwa kuingiza mashabiki katika mchezo wetu. Tunasema pigo kwa kuwa tunafahamu nguvu kubwa ya mashabiki wanapokuwepo uwanjani. Hao mashabiki bora ambao tunajinasibu nao hawatakuwepo uwanjani Jumapili hii."

"Nitumie nafasi hii kuwambia kwamba taarifa ilikuja jana mchana na saa 11 jioni tukatoa taarifa ya kusitisha kuuza tiketi. Juzi wakati tunatangaza kuuza tiketi hadi jana asubuhi tulikuwa hatujapokea taarifa"

"Sisi Simba Sports tunayo masikitiko makubwa mno kucheza mchezo huu muhimu bila mashabiki, tunaumia sababu tunafahamu thamani ya mashabiki kwa Simba kupata mafanikio"

"Taarifa sahihi ni tumefungiwa mechi moja, mechi ya robo fainali tutacheza na mashabiki na tayari sisi tumeshafuzu. Baada ya hukumu kutoka yameibuka maoni mengi ya mashabiki wakitaka ushirikishwaji kwa kuwa kosa hili ambalo limetokea ni la Wanasimba wote, asitokee wa kumnyoshea kidole mwenzake," alisema Ahmed


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.