Mpole apewa jukumu la kuibeba Kagera Sugar

Joel JJ By Joel JJ β€’ 23rd January 2025


Mpole apewa jukumu la kuibeba Kagera Sugar

Kocha wa Kagera Sugar, Melis Medo ameonyesha imani kubwa kwa mshambuliaji mpya, George Mpole, akisema ana uwezo wa kufanya mambo makubwa na kuwa msaada katika juhudi zao za kujinasua kutoka kwenye hatari ya kushuka Ligi Kuu Bara

Medo amesema kwamba Mpole atakuwa silaha muhimu katika timu hiyo hasa katika duru la pili la Ligi Kuu Bara ambapo Kagera Sugar inakutana na changamoto kubwa ya kupigania kubaki kwenye ligi

Mpole ambaye amejiunga na Kagera Sugar akitokea Pamba Jiji katika dirisha dogo lililofungwa Januari 15 ni mchezaji mwenye rekodi nzuri akiwahi kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara 2021/22 baada ya kufunga mabao 17

Medo alisema anaamini uzoefu wa Mpole utaongeza nguvu katika timu yake ambayo inashika nafasi ya 15 kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 11

"George Mpole ni mshambuliaji ambaye ana uzoefu mkubwa na amewahi kuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu Bara. Ana uwezo wa kuleta madhara makubwa katika maeneo muhimu uwanjani. Hii ni silaha muhimu kwa timu yetu kwani tunahitaji mchezaji ambaye anaweza kuleta ubunifu mbele na kumalizia nafasi za kufunga" 

"Tunahitaji wachezaji kama yeye ambao hawana hofu wanapambana hadi dakika ya mwisho na wanajua jinsi ya kutumia nafasi. Huu ndio ubora tunaohitaji ili kujinasua katika nafasi tuliyopo sasa,” alisema Medo

Mbali na Mpole, Kagera Sugar pia imetambulisha nyota mwingine katika dirisha lililofungwa la usajili ambaye ni kipa Ahmed Feruzi aliyejiunga kwa mkopo akitokea Simba, na Medo anaamini kuwa kuongezwa kwa kipa huyo kutaimarisha safu ya ulinzi ya timu hiyo

Mwanaspoti


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.