Kocha Mkuu wa Yanga Sead Ramovic amesema hawakuwa na bahati kufuzu robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa lakini sasa wanafanya kazi kubwa katika uwanja wa mazoezi ili kujiimarisha na kuwa bora zaidi
Akizungumza baada ya mchezo wa CRDB Cup dhidi ya Copco Fc jana ambao Wananchi waliibuka na ushindi wa mabao 5-0, Ramovic aliwapongeza wachezaji wake kwa ushindi huo na pia akazungumzia kwa ufupi nini anafanya katika uwanja wa mazoezi ili Yanga iendelee kucheza kwa kasi na ari kubwa
"Nawapongeza wachezaji wangu kwa ushindi huu, matokeo haya ni mwendelezo wa dhamira yetu ya kucheza aina ya soka la ushindani lenye 'intensity' ya juu"
"Tunafanya mazoezi ya kukimbia na kuimarisha utimamu wa wachezaji wetu ili kuhakikisha wanacheza aina hii ya soka"
"Baada ya kutolewa katika ligi ya mabingwa nilisema kuhusu wachezaji wangu kukosa utimamu wa kucheza aina hii ya soka bahati mbaya baadhi ya waandishi wa habari hawakunielewa wakasema naidharau ligi ya Tanzania jambo ambalo si kweli"
"Mimi nilikuwa nazungumzia timu yangu ya Yanga na kile tunapaswa kuboresha ili kuwa na ushindani katika ligi ya mabingwa"
"Lengo langu ni kuona Yanga inaweza kucheza nusu fainali na hata kutwaa taji la ligi ya mabingwa. Naamini tuko katika njia sahihi na tutafikia malengo yetu," alisema Ramovic



