Kikosi cha Simba kitaelekea mkoani Tabora Jumamosi ya Februari 1 tayari kwa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Tabora United utakaopigwa Jumapili, Februari 02 katika uwanja wa Ali Hassan Mwinyi
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba Ahmed Ali amesema tayari timu imerejea mazoezini kujiandaa na mchezo huo mgumu lakini muhimu kwa Simba kushinda ili kuzidi kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi
Ahmed amesema Simba inatambua ugumu wa mchezo huo hasa ikizingatiwa Tabora United walizifunga timu nyingine shindani
"Timu imerejea mazoezini baada ya mchezo wa kombe la CRDB dhidi ya Kilimanjaro Wonders. Wachezaji wote wamerejea ikiwa ni pamoja na wale waliokuwa wamepewa mapumziko na wengine kupewa ruhusa kusafiri nje ya nchi kuona familia zao"
"Timu itaondoka Dar es salaam siku ya Jumamosi, Februari 1 kuelekea Tabora kwa ajili ya mchezo dhidi ya Tabora United utakaopigwa Jumapili, Februari 2"
"Tunatambua hautakuwa mchezo mwepesi kwani Tabora United wameimarika sana ukilinganisha na tulivyocheza nao mara ya kwanza na kuwafunga mabao 4-0"
"Wamepata ushindi dhidi ya timu zinazoshika nafasi ya pili na tatu, hivyo wanaona kama wanaweza kuifunga Simba pia"
"Lakini niwaambie Simba ni timu tofauti na imara zaidi kuliko hizo timu walizozifunga na ndio maana iko kileleni mwa msimamo wa ligi. Hivyo sisi tutakwenda Tabora tukiwa na matumaini makubwa ya kushinda siku ya Jumapili," alisema Ahmed



