Kikosi cha Simba leo kinahamishia mawindo yake katika uwanja wa Benjamin Mkapa kuikabili Azam Fc kwenye mwendelezo wa ligi kuu ya NBC
Ni Mzizima Derby, moja ya mechi ngumu ambayo matokeo yake yanaweza kuiweka Simba katika nafasi nzuri kwenye mbio za ubingwa au kuvuruga hesabu ingawa bado ni mapema kwa sababu kuna mechi nyingi za kuchezwa
Hata hivyo Azam Fc ni miongoni mwa timu shindani katika mbio za ubingwa hivyo kama Simba itachukua alama tatu dhidi yao ni wazi zitakuwa na thamani kubwa
Licha ya Simba kushinda mabao 2-0 katika mchezo wa duru ya kwanza uliopigwa visiwani Zanzibar, takwimu zinaonyesha mechi kati ya Simba dhidi ya Azam Fc haijawahi kuwa nyepesi
Simba imekuwa na msimu bora mpaka sasa, ikifanya vizuri ligi ya ndani na Kimataifa, bado inaonekana kuwa na nafasi nzuri ya kuibuka na ushindi leo
Baada ya kukosa ushindi katika mchezo uliopita dhidi ya Coastal Union, leo Azam Fc inahitaji kushinda ili kuweka hai malengo yao katika mbio za ubingwa
Ni wazi kama Azam Fc itafungwa leo, pengine watahitaji kubadili malengo yao ya msimu huu kwani haitakuwa rahisi kwao tena kuwa bingwa
Sasa inashika nafasi ya tatu ikiwa na alama 43 wakati Yanga iko kileleni ikiwa na alama 55 huku Simba ikishika nafasi ya pili ikiwa na alama 50
Baada ya mechi ya leo Azam Fc watasalia na mechi 9 wakati Simba itakuwa na mechi 10



