Kocha Mkuu wa Yanga Miloud Hamdi amesema kikosi chake kiko tayari kwa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Simba ambao utapigwa kesho Jumamosi katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Akizungumzia maandalizi ya mchezo huo utakaopigwa saa 1:15 usiku, Hamdi amesema anaiheshimu klabu ya Simba na hii ni mechi kubwa lakini anaamini ubora wa timu yake unakwenda kuamua mchezo huo
"Nafurahi kuwa hapa na klabu ya Yanga na zaidi kucheza mechi hii ya derby katika miongoni mwa mechi kubwa Afrika. Hii haitakuwa mara ya kwanza kushiriki mchezo mkubwa wa aina hii lakini kwa hapa Tanzania hii ni derby yangu ya kwanza na matarajio yangu ni kupata ushindi"
"Tunajua kesho ni mechi ya kipekee kulinganisha na mechi nyingine. Nafurahi nimepata siku tano za kuiandaa timu yangu kuelekea mchezo huu. Jambo muhimu ni kuwa tumefanya maandalizi mazuri na tunaamini mechi hii mchezo wa mpira wa miguu utashinda"
"Natarajia kuona mchezo wa wazi kila timu ikijaribu kushinda, tunapaswa kuwa bora kimbinu na kutumia vyema nafasi tutakazotengeneza. Najua Simba ni timu imara, nimesema lazima tuwe bora kimbinu, tumeandaa mazingira yote ya mchezo naamini tutafanya kitu kizuri," alisema Hamdi
Hamdi amesisitiza hana hofu yoyote kuelekea mchezo huo kwani anaamini uwezo wa timu yake na zaidi mchezo wa mpira wa miguu ni burudani
"Kama kocha sina wasiwasi wowote kuelekea mchezo huu, sisi ni Yanga, timu kubwa Afrika hatuwezi kuhofia mechi hii. Naamini wachezaji wangu watapambana ili kuwapa furaha mashabiki wetu," alisema Hamdi



