Kocha Mkuu wa Simba Fadlu Davids ana matumaini ya kufanya vizuri katika mchezo wa robo fainali kombe la Shirikisho dhidi ya Al Masry ambapo mechi ya mkondo wa kwanza itapigwa April 02 huko Misri na marudiano kupigwa dimba la Benjamin Mkapa April 09
Fadlu amesema kikosi chake sasa kimeimarika tofauti na walivyoanza msimu, wanajua watakabiliwa na mechi ngumu Misri lakini watahitaji kupambana na muhimu angalau wafunge bao la ugenini
"Tutakwenda Misri huku tukifahamu haitakuwa mechi nyepesi ugenini lakini nafurahi kuona wachezaji wangu sasa wako tayari na wanafahamu mazingira ambayo tutakutana nayo"
"Tuna timu changa yenye wachezaji wengi ambao hawana uzoefu na michuano ya Kimataifa, lakini mechi za hatua ya awali na makundi zimesaidia kuwaimarisha kwa kiasi kikubwa"
"Kumaliza nafasi ya kwanza katika hatua ya makundi ni jambo kubwa ambalo limetuongezea kujiamini kuelekea hatua hii inayofuata"
"Tutapaswa kucheza kwa umakini mkubwa ugenini ili tuwe na nafasi ya kusonga mbele katika mechi ya pili tutakayocheza nyumbani. Malengo yetu ni kuona tunafika mbali katika michuano hii," alisema Fadlu
Aidha Fadlu amebainisha kuwa mafanikio ya timu yake hayapaswi kutegemea mchezaji mmoja, kila mchezaji katika kikosi chake ana umuhimuΒ
Amesema ili kufanya vizuri katika michuano yote wanayoshiriki, ni lazima kuwa na kikosi kipana ambacho kitatoa nafasi kwa kila mchezaji
"Wakati niko Orlando Pirates, tulicheza fainali ya kombe la Shirikisho 2022/23 lakini hatukuwa na kikosi kipana, tulitumia wachezaji walewale katika kila mechi"
"Hili ilitusumbua sana kwenye ligi baada ya michuano ya CAF kumalizika, kama tunataka kufanya vizuri katika mashindano yote lazima tuwe na uwiano mzuri kitimu"
"Kila mchezaji hapa ana nafasi ya kuchangia mafanikio ya timu na sio kutegemea mchezaji mmoja," aliongeza Fadlu