Yanga imeendelea kujiimarisha kileleni mwa msimamo wa ligi baada ya kuichapa Azam Fc mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Azam Complex
Yanga iliuanza mchezo huo kwa kasi ikionyesha dhamira ya kusaka ushindi mapema na alikuwa Pacome Zouzoua aliyefunga bao la kwanza dakika ya 11 akimalizia kazi ya Prince Dube
Mabingwa hao watetezi waliendelea kutawala mchezo katika kipindi cha kwanza wakitengeneza nafasi nyingi lakini mlinda lango wa Azam Fc Zuberi Foba alikuwa kikwazo akiokoa michomo ya hatari
Alikuwa ni Prince Dube aliyewaadhibu waajiri wake hao wa zamani akifunga bao la pili dakika ya 34 akimalizia pasi ya Mudathir Yahya
Yanga ilikwenda mapumziko ikiwa na uongozi wa mabao 2-0. Kipindi cha pili Wananchi waliendelea kutawala mchezo lakini wakati mchezo ukielekea ukiongoni kasi yao ilipungua na kuwapa nafasi Azam Fc kurejea mchezoni
Lusajo Mwaikenda akafunga bao la kufutia machozi kwa upande wa Azam Fc akimalizia kona ya Feisal Salum
Hata hivyo Wananchi walifanikiwa kulinda uongozi wao hadi pale mwamuzi Ahmed Arajiga alipomaliza mchezo
Yanga imefikisha alama 67 sasa ikiongoza ligi kwa tofauti ya alama 10 huku ikisaliwa na mechi nne tu kuhitimisha msimu
Ni ushindi muhimu kwa Yanga ambao kwa hakika unawaweka katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa
Aidha ushindi huo unaihakikishia Yanga kukata tiketi ya kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa msimu ujao kwani Wananchi sasa wana uhakika wa kumaliza nafasi mbili za juu