Majeraha kumuweka nje Pacome wiki mbili

Joel JJ By Joel JJ β€’ 15th April 2025


Majeraha kumuweka nje Pacome wiki mbili

Kiungo mshambuliaji wa Klabu ya Yanga, Pacome Zouzoua, anakabiliwa na mapumziko ya takribani wiki mbili nje ya dimba baada ya kuumia kifundo cha mguu katika mchezo wa Ligi Kuu ya NBC dhidi ya Azam FC

Mchezo huo uliochezwa hivi karibuni uliisha kwa Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, huku Zouzoua akiwa mmoja wa wafungaji na bao lingine likifungwa na Prince Dube

Hata hivyo, licha ya mchango wake mkubwa katika ushindi huo, Zouzoua hakumaliza dakika 90 baada ya kupata jeraha la kifundo cha mguu (ankle sprain) ambalo liliwalazimu benchi la ufundi kumtoa uwanjani

Daktari wa Yanga, Moses Etutu, amethibitisha jeraha hilo na kueleza kuwa mchezaji huyo raia wa Ivory Coast atakuwa nje ya uwanja kwa muda wa siku 10 hadi 14

"Pacome aliumia kifundo cha mguu, matarajio ni kwamba atakuwa nje kwa siku 10 hadi 14. Maendeleo yake ya awali ni mazuri, na iwapo atazingatia kwa makini maagizo ya kitabibu, kuna uwezekano akapona mapema au kuchelewa kwa siku chache zaidi," alisema Dkt. Etutu.

Hili ni tukio la pili kwa Zouzoua kupata jeraha kama hilo katika mechi dhidi ya Azam FC. Katika msimu uliopita, alikumbwa na jeraha la aina hiyo hiyo kwenye mchezo wa ligi ambao Yanga walipoteza kwa mabao 2-1

Inaonekana kuwa mechi dhidi ya Azam FC imekuwa na historia isiyo nzuri kwa kiungo huyo fundi wa mpira

Mashabiki wa Yanga bila shaka watamkosa Zouzoua, hasa ikizingatiwa mchango wake mkubwa katika safu ya ushambuliaji

Habari njema ni kuwa huenda akakosa mechi mbili tu. Leo hatakuwa sehemu ya kikosi kitakachoikabili Stand United katika mchezo wa robo fainali ya kombe la CRDB na pia atakosa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Fountain Gate April 20


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.