Klabu ya Azam FC, inayojulikana kama matajiri wa Jiji la Dar es Salaam, imekuwa na msimu wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara wa 2024/25 uliojaa mchanganyiko wa mafanikio na changamoto
Hata hivyo, licha ya juhudi zao na ubora wa kikosi, timu hiyo haitafanikiwa kufikia kiwango cha pointi ilichokifikia msimu uliopita.
Katika msimu wa 2023/24, Azam FC ilimaliza ligi katika nafasi ya pili ikiwa na pointi 69—rekodi nzuri ambayo iliwafanya kuwa washindani wakuu wa Yanga SC, waliotwaa ubingwa kwa pointi 80. Lakini msimu huu hali ni tofauti.
Mpaka sasa, Azam FC iko nafasi ya tatu ikiwa na pointi 51 baada ya kucheza michezo 26. Imeweza kushinda mechi 15, kutoa sare sita na kupoteza tano. Kwa hesabu rahisi, hata wakishinda michezo yote minne iliyosalia, watafikisha pointi 63 tu—sita pungufu ya msimu uliopita.
Hali hii inaonesha wazi kuwa, licha ya uwekezaji mkubwa na kuwa na wachezaji wenye viwango bora, bado Azam FC haijafanikiwa kuendeleza uthabiti wa matokeo kama ilivyofanya msimu uliopita. Tatizo linaweza kuwa ni ukosefu wa muendelezo wa ushindi, majeraha kwa wachezaji muhimu, au pengine presha ya ushindani mkali kutoka kwa washindani wake Yanga SC na Simba SC.
Mashabiki na wadau wa soka wanaamini kuwa Azam FC bado ni timu yenye uwezo mkubwa, lakini inahitaji kufanya tathmini ya kina mwishoni mwa msimu huu ili kubaini wapi walikosea na nini kinapaswa kufanyiwa kazi kuelekea msimu ujao



