Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imechukua hatua madhubuti katika kukabiliana na changamoto ya kujaa maji katika eneo la kuchezea la Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam
Hatua hii imekuja kufuatia tukio la Aprili 09, ambapo uwanja huo ulikumbwa na changamoto ya maji kujaa baada ya mvua kunyesha muda mfupi kabla ya mchezo wa Kombe la Shirikisho la CAF kati ya Simba SC na Al Masry ya Misri.
Kutokana na hali hiyo, Serikali ilitangaza kufungia rasmi uwanja huo kwa muda ili kufanikisha ukarabati na maboresho muhimu yanayolenga kuboresha miundombinu ya mfumo wa mifereji ya maji na kuhakikisha eneo la kuchezea linabaki katika hali bora hata wakati wa mvua.
Akizungumza kuhusu hatua zilizochukuliwa, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Gerson Msigwa alisema:
"Serikali imeleta wataalam kutoka nchini Uturuki kwa ajili ya kukabiliana na changamoto zilizojitokeza kwenye eneo la kuchezea, na itakuwa sawa hivi karibuni tu."
Watalaam hao kutoka Uturuki wameshaanza kazi ya tathmini na matengenezo maalum kwenye eneo la uwanja, wakiwa na uzoefu mkubwa wa kushughulikia changamoto za aina hiyo katika viwanja mbalimbali duniani
Uwepo wao unaleta matumaini makubwa kwa wadau wa michezo nchini, hasa kwa timu zinazotegemea uwanja huo kwa mechi za kimataifa na za ligi ya ndani.
Aidha, Serikali inaendelea na ukarabati mwingine wa sehemu mbalimbali za uwanja huo, ikiwa ni pamoja na viti vya watazamaji, mfumo wa taa na maeneo ya vyumba vya kubadilishia nguo ili kuhakikisha viwango vya kimataifa vinazingatiwa.
Hatua hii ni sehemu ya dhamira ya dhati ya Serikali katika kuboresha miundombinu ya michezo nchini, kuleta mazingira bora kwa wachezaji na watazamaji, na kuifanya Tanzania kuwa mwenyeji wa mashindano ya kimataifa kwa ufanisi zaidi.