Klabu ya Simba imeitangaza Jayrutty Investment Company Limited kushinda tenda ya usambazaji wa jezi za klabu ya Simba kwa kipindi cha miaka mitano
Mwenyekiti wa Kamati ya Tenda Dkt. Seif Muba amesema kampuni hiyo imeweka kiasi cha fedha Tsh. 38 Bilioni ambapo klabu ya Simba inakwenda kupata Tsh. 5.6 Bilioni kwa mwaka
Aidha katika kipindi cha miaka mitano, kampuni hiyo itaboresha miundo mbinu ikiwa ni pamoja na kununua basi jipya, kujenga uwanja utakaochukua kati ya mashabiki 10,000-12,000, kujenga ofisi rasmi za klabu na studio kwa ajili ya kitengo cha habari na Mawasiliano
"Tulipokea barua nyingi za maombi lakini bodi iliamua makampuni yashindane kwa tenda. Kampuni nane zilichukua tender document lakini kampuni sita zilirudisha document. Maombi ya wazabuni yalifunguliwa kwa uwazi na baada ya mchakato wazabuni wote walijulishwa mzabuni ambaye ameibuka mshindi kwa kuweka fedha na vitu vingi ambavyo tulihitaji. Tuliingia mkataba wa miaka mitano na kampuni hiyo"
"Mshindi aliyeshinda tenda hiyo ameshinda kwa kuweka kiasi cha fedha cha Tsh. 38 Bilioni. Napenda kuitangaza kampuni ya Jayrutty Investment Company Limited kama mshindi. Klabu ya Simba inakwenda kupata Tsh. 5.6 Bilioni kwa mwaka," alisema Muba
Mkurugenzi wa Jayrutty Investment Company Limited, CPA Joseph Rwegasira amesema tayari kampuni hiyo imetoa asilimia 30% ya kiasi cha fedha ambazo wanapaswa kutoa katika mwaka wa kwanza wa tenda hiyo
"Kiasi ambacho kimetajwa ni kiasi ambacho tumezingatia mambo mengi kama klabu. Nipende kuwahakikishia kabla hata hatujafanya kitu chochote tumeshaweka 30% ya hiki kiasi cha mwaka wa kwanza."
"Jambo la kwanza ambalo tunakwenda kutekeleza ni kujenga uwanja wa mpira, uwanja ambao utachukua mashabiki 10,000 hadi 12,000 na tumekubaliana kwamba Simba wana uwanja Bunju na tutakwenda kujenga uwanja Bunju lakini kama watakuja na mapendekezo mengine basi tutayafata"
"Simba ni timu kubwa Afrika na sisi tumesema kwamba tutanunua basi jipya la Irizar, kila kitu kipo sawa. Muda si mrefu mtaliona hapa. Tutaangalia pia upande wa media, tunakwenda kujenga media kubwa kama klabu zingine kubwa na tumeshaanza utaratibu."
"Tunajua kwamba Simba makao makuu yapo Msimbazi lakini tunakwenda kujenga ofisi za kisasa. Lakini pia kila mwaka tutatoa Tsh. 100 milioni ya kusaidia kukuza soka la vijana. Kila mwaka pia tutachangia Tsh. 100 milioni kuchangilia pre season. Pia tumeahidi kujenga kituo maalumu cha matibabu ya wachezaji. Kila mwaka pia tutashiriki bega bega katika Simba Day, tutachangia Tsh. 100 milioni kila mwaka."
"Hizi ni baadhi ya faida za ziada ambazo sisi tutatoa kwa Simba Sports Club. Kila mwaka tumekubali kutoa Tsh. 470 milioni kwa wachezaji, uongozi utagawa kwa namna ambayo wataona inafaa na hii fedha itakuwa inaongezeka kila mwaka."
"Tumeenda kimataifa kuhakikisha tunapata international brand, niwahakikishie kwamba msimu unaokuja jezi ambayo Simba watavaa, watavaa jezi ya kimataifa. Tumeingia mkataba wa kimataifa na brand mojawapo kubwa duniani ambayo inazivisha klabu nyingi kubwa," alisema Mwanzilishi na Mwenyekiti wa Jayrutty Investment Company Limited, CPA Joseph Rwegasira