Leo, Jumamosi tarehe 19 April 2025, Afrika Kusini inakuwa mwenyeji wa mechi mbili za nusu fainali za Ligi ya Mabingwa Afrika, ambapo timu kutoka Afrika Kusini zitakabiliana na wapinzani kutoka Misri.
Mamelodi Sundowns wataikaribisha Al Ahly katika uwanja wa Loftus Versfeld, Pretoria. Hii ni mara nyingine timu hizi mbili zinakutana katika hatua ya mtoano, huku historia ya mechi zao ikionyesha ushindani mkubwa. Katika mechi tisa zilizopita, kila timu imeshinda mara tatu na sare tatu zimetokea
Sundowns wameonyesha ubabe katika michuano ya msimu huu, wakifunga mabao 21 katika mechi tano, wastani wa mabao 4.2 kwa mchezo, huku wakiruhusu mabao manne tu . Kwa upande mwingine, Al Ahly wamefunga mabao tisa na kuruhusu matatu katika mechi tano, wakionyesha uimara wa safu yao ya ulinzi
Hata hivyo, Al Ahly wanakabiliwa na presha kubwa kutokana na matokeo yasiyoridhisha hivi karibuni na ukosoaji kwa kocha wao, Marcel Koller. Sundowns, licha ya kuwa na historia ya kushindwa katika hatua za mtoano, wanatarajia kutumia faida ya uwanja wa nyumbani kupata ushindi muhimu kabla ya mchezo wa marudiano wiki ijayo mjini Cairo
Katika mchezo mwingine wa nusu fainali, Orlando Pirates watawakaribisha Pyramids FC katika uwanja wa Orlando, Soweto. Pirates wamekuwa na msimu mzuri, wakimaliza hatua ya makundi bila kupoteza mechi yoyote na kushinda mechi tatu ugenini Afrika Kaskazini
Kocha wao, Jose Riveiro, raia wa Hispania, ameisuka upya timu hiyo tangu kujiunga nao mwaka 2022, akiiongoza kushinda mataji matano ya ndani na kuifanya kuwa tishio katika soka la Afrika
Pyramids, licha ya kuwa na historia fupi tangu kuanzishwa mwaka 2008, wamepiga hatua kubwa katika soka la Afrika, wakitarajia kushinda taji lao la kwanza la ligi ya Misri msimu huu. Mechi hii inatarajiwa kuwa na ushindani mkali, huku Pirates wakilenga kupata ushindi nyumbani kabla ya mchezo wa marudiano mjini Cairo.
Mechi hizi za nusu fainali zinaweka jukwaa la fainali ya kuvutia kati ya timu kutoka Afrika Kusini na Misri. Mashabiki wa soka barani Afrika wanatarajia burudani ya hali ya juu kutoka kwa timu hizi nne zinazowania taji la Ligi ya Mabingwa Afrika.



