Katika kile kinachotarajiwa kuwa mchezo wa kuvutia na wenye ushindani mkali, Simba SC ya Tanzania inawakaribisha wageni kutoka Afrika Kusini, Stellenbosch FC, kwenye uwanja wa kihistoria wa New Amaan Complex kwa ajili ya mechi ya kwanza ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF (CAF Confederation Cup)
Ni mechi kubwa na muhimu kwa Simba kushinda ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kutinga fainali ya michuano hiyo na kurudia kile walichofanya mwka 1993
Wakicheza mechi ya Kimataifa kwa mara ya kwanza visiwani Zanzibar, Simba inatarajiwa kupata sapoti kubwa ya mashabiki ambapo dimba la New Amaan Complex linatarjiwq kuwa 'full house'
Kwa kuwa ni mechi ambayo Simba inahitaji kushinda nyumbani, Kocha Fadlu Davids ni wazi ataingia na mfumo wake wa kushambulia, akimtegemea mshambuliaji Steven Mukwala kuongoza mashambulizi
Mganda huyo atasaidiana na Elie Mpanzu, Kibu Denis, na Jean Charles Ahoua huku eneo kati likitarajiwa kuwa chini ya usimamizi wa viungo Fabrice Ngoma na Yusuf Kagoma
Safu ya ulinzi itaendelea kuwa imara ikiongozwa na wazoefu Shomari Kapombe, Mohammed Hussein, Abdulrazak Hamza, na Carabou Chamou, huku Simba wakitarajiwa kutumia kwa ustadi faida ya kucheza nyumbani
Hata hivyo ni wazi haitakuwa mechi nyepesi kwani licha ya Stellenbosch kuwa wageni wapya kwenye michuano ya kimataifa, wamewashangaza wengi kwa kiwango chao bora msimu huu
Timu hiyo ya Afrika Kusini imeonesha ubora mkubwa, hasa walipowang'oa mabingwa watetezi Zamalek katika hatua ya robo fainali β kitendo kilichowafanya kuchukuliwa kwa uzito mkubwa sasa
Simba leo inapaswa kumaliza mechi nyumbani kwa kuibuka na ushindi mnono ili kuwa na kazi rahisi ya kukamilisha mpango wa kutinga fainali pale watakaposafiri Afrika Kusini kwa mechi ya marudiano wiki ijayo



