Yanga yaipania Fountain Gate NBC PL

Joel JJ By Joel JJ β€’ 21st April 2025


Yanga yaipania Fountain Gate NBC PL

Kuelekea mchezo wa ligi kuu ya NBC kati ya Fountain Gate dhidi ya Yanga ambao utapigwa leo Jumatatu, April 21 katika uwanja wa Tanzanite Kwaraa Manyara, Kocha Mkuu wa Yanga Miloud Hamdi amesema wamejipanga kushinda mchezo huo ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kutetea ubingwa

Aidha Hamdi ambaye ameiongoza Yanga katika mechi 11 akishinda 10 na kutoka sare mechi moja, amesema amekiandaa kikosi chake kimbinu kuikabili Fountain Gate

Amesema anaamini wachezaji wake watatafsiri vyema mpango wa mchezo huo na kuibuka na ushindi

"Lazima tuwe makini sana, tushinde kila mechi. Pia, tumefanya mikutano ya kiufundi, tumeangalia video na kufanya mazoezi ya kiufundi ili kujiandaa vizuri"

"Ninawaambia mara nyingi nyota wa mchezo ni mfumo. Wachezaji wote wakielewa mfumo, tutashinda mechi nyingi. Tuna wachezaji wenye uwezo wa kufanya mfumo ufanye kazi lakini jambo la kwanza ni kuelewa mfumo"

"Kwa hiyo mchezaji anapobadilishwa au kuingia uwanjani, lazima ajue moja kwa moja anachotakiwa kufanya na kile asichopaswa kufanya na kuelewa wa Wachezaji wangu naamini tutaendelea kufanya vizuri kwenye kila mchezo," alisema

Aidha, Hamdi amekiri baadhi ya wachezaji wake wana changamoto za majeruhi na maumivu ya hapa na pale lakini amesema yeye anaamini ana timu imara na ataendelea na utaratibu wa kumpa nafasi kila mchezaji

"Ni kweli tuna baadhi ya wachezaji majeruhi kama Aucho, Pacome bado hajawa tayari, Musonda anahisi maumivu kidogo si makubwa lakini hatuwezi kumuhatarisha pamoja na Azizi Ki ana maumivu ya muda mrefu"

"Nawaheshimu wachezaji wote. Mimi si kocha wa kulalamika kwamba sina huyu au yule hapana nitampa nafasi kila mchezaji. Hiyo ndiyo njia pekee ambayo itatuwezesha kufika mwezi Mei tukiwa imara, kwa sababu kila mchezaji atakuwa amepewa muda wa kucheza. Hilo ni jambo muhimu sana kwangu," aliongeza Hamdi


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.