Ni JKU vs Yanga, fainali Muungano Cup

Joel JJ By Joel JJ β€’ 1st May 2025


Ni JKU vs Yanga, fainali Muungano Cup

Kikosi cha Yanga usiku wa leo Alhamisi kitakuwa uwanjani kuwakabili JKU ya Zanzibar katika fainali ya Kombe la Muungano

Yanga iliponea chupuchupu katika hatua ya nusu fainali ambapo ililazimika kusubiri hadi hatua ya penalti baada ya dakika 90 za pambano hilo kuisha kwa sare ya 1-1, leo inavaana na JKU ambao ni watetezi wa Ligi Kuu Zanzibar

Yanga, wanaoshikilia ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa msimu wa tatu mfululizo kwa sasa itashuka uwanjani kuvaana na mabingwa wenzao wa Zanzibar, JKU iliyowatoa nishai Azam FC kwa kuifunga mabao 2-1 katika mchezo mwingine wa nusu fainali

Timu hizo ndizo mabingwa wa Ligi za Tanzania Bara na Zanzibar na leo itakuwa mechi ya kibabe kusaka mkali wao kwa Muungano

Timu zote zitashuka kwenye Uwanja wa Gombani kuanzia saa 1:15 usiku kila moja ikiwa na lengo tofauti, Yanga ikitaka kuboresha rekodi ya kubeba mara nyingi taji la michuano hiyo, lakini JKU ikisaka ubingwa wa kwanza kwani haijawahi kutwaa taji hilo na hizi ni fainali za kwanza kwao

Rekodi zinaonyesha tangu kuanzishwa kwa michuano hiyo 1982, Yanga imetwaa mara sita miaka ya 1983, 1987, 1991, 1996, 1997 na 2000

Yanga inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu ikisaka taji la msimu wa nne mfululizo, inahitaji kushinda ili kufikisha taji la saba

Kocha wa Yanga, Miloud Hamdi amesisitiza kwamba anahitaji kubeba kombe hilo ili kuwaweka sawa wachezaji kabla ya kumalizana na mechi za Ligi Kuu na nusu fainali ya Kombe la Shirikisho (FA)


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.