Kikosi cha Yanga usiku wa leo Alhamisi kitakuwa uwanjani kuwakabili JKU ya Zanzibar katika fainali ya Kombe la Muungano
Yanga iliponea chupuchupu katika hatua ya nusu fainali ambapo ililazimika kusubiri hadi hatua ya penalti baada ya dakika 90 za pambano hilo kuisha kwa sare ya 1-1, leo inavaana na JKU ambao ni watetezi wa Ligi Kuu Zanzibar
Yanga, wanaoshikilia ubingwa wa Ligi Kuu Bara kwa msimu wa tatu mfululizo kwa sasa itashuka uwanjani kuvaana na mabingwa wenzao wa Zanzibar, JKU iliyowatoa nishai Azam FC kwa kuifunga mabao 2-1 katika mchezo mwingine wa nusu fainali
Timu hizo ndizo mabingwa wa Ligi za Tanzania Bara na Zanzibar na leo itakuwa mechi ya kibabe kusaka mkali wao kwa Muungano
Timu zote zitashuka kwenye Uwanja wa Gombani kuanzia saa 1:15 usiku kila moja ikiwa na lengo tofauti, Yanga ikitaka kuboresha rekodi ya kubeba mara nyingi taji la michuano hiyo, lakini JKU ikisaka ubingwa wa kwanza kwani haijawahi kutwaa taji hilo na hizi ni fainali za kwanza kwao
Rekodi zinaonyesha tangu kuanzishwa kwa michuano hiyo 1982, Yanga imetwaa mara sita miaka ya 1983, 1987, 1991, 1996, 1997 na 2000
Yanga inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu ikisaka taji la msimu wa nne mfululizo, inahitaji kushinda ili kufikisha taji la saba
Kocha wa Yanga, Miloud Hamdi amesisitiza kwamba anahitaji kubeba kombe hilo ili kuwaweka sawa wachezaji kabla ya kumalizana na mechi za Ligi Kuu na nusu fainali ya Kombe la Shirikisho (FA)



