Kocha Msaidizi wa Simba Selemani Matola amesema wamejipanga kuibuka na ushindi katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya KMC ambao utapigwa leo Jumapili katika uwanja wa KMC Complex licha ya ratiba ngumu inayowakabili
Akizungumza katika Mkutano na wanahabari jana, Matola alisema wamekosa muda wa kutosha wa maandalizi ya mechi kutokana na ratiba inayowalazimu kucheza kila baada ya siku tatu
Matola amesema wanajivunia kuwa na kikosi kipana kwani licha ya mabadiliko wanayofanya katika kila mechi, wameendelea kuibuka na ushindi
"Ratiba yetu ni ngumu kwani hatupati muda wa kutosha wa maandalizi lakini tuna kikosi kipana ambacho kinatuwezesha kupata ushindi popote"
"Tunafahamu mchezo dhidi ya KMC utakuwa mgumu lakini sisi tumejipanga kuhakikisha tunapata matokeo chanya," alisema Matola
Simba leo inacheza mechi ya nne katika kipindi cha siku 10 ikishinda mechi tatu zilizopita dhidi ya Mashujaa Fc (2-1), JKT Tanzania (1-0) na Pamba Jiji (5-1)
Baada ya mchezo dhidi ya KMC, Simba itasafiri Morocco kumenyana na RS Berkane katika mchezo wa mkondo wa kwanza fainali ya kombe la Shirikisho (CAF CC) utakaopigwa May 17



