Ni RS Berkane dhidi ya Simba, fainali ya kwanza leo

Joel JJ By Joel JJ • 17th May 2025


Ni RS Berkane dhidi ya Simba, fainali ya kwanza leo

Leo Jumamosi, Mei 17, macho ya mashabiki wa soka barani Afrika yatakuwa yakielekezwa katika Uwanja wa Manispaa ya Berkane, Morocco, ambako klabu ya Simba SC ya Tanzania itachuana na RS Berkane ya Morocco kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza wa fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAF Confederation Cup). Mchezo huo utapigwa saa 4 usiku kwa saa za Afrika Mashariki.

Hii ni mara ya pili kwa Simba kufika katika fainali ya mashindano ya CAF, baada ya kufanya hivyo mwaka 1993 kwenye Kombe la CAF, ambapo waliambulia patupu dhidi ya Stella Abidjan ya Ivory Coast. Katika fainali hiyo ya awali, Simba ilianza kwa suluhu ugenini kabla ya kupoteza kwa mabao 2-0 kwenye mechi ya marudiano jijini Dar es Salaam. Safari hii, kikosi cha kocha Fadlu Davids kimepania kuandika historia mpya kwa kulinyakua taji la kwanza la kimataifa baada ya zaidi ya miongo mitatu ya kusubiri.

Nafasi ya Simba

Simba imekuwa ikionyesha mwelekeo chanya msimu huu, ikiimarika hatua kwa hatua na kufika hatua ya fainali huku ikionekana kuwa miongoni mwa timu bora barani Afrika, jambo linalothibitishwa na kushika nafasi ya nne katika viwango vya CAF. Kikosi cha Msimbazi kinaingia kwenye mchezo huu kikiwa na matumaini makubwa, lakini pia kikiwa na tahadhari dhidi ya wapinzani wao waliozoea presha ya fainali.

Katika mchezo wa leo, Simba italenga kupata matokeo mazuri – ushindi, sare au hata kama itapoteza basi isiwe kwa tofauti kubwa ya mabao. Jambo la msingi zaidi kwa vijana wa Fadlu Davids ni kuhakikisha wanarudi Dar es Salaam wakiwa na bao la ugenini, ambalo linaweza kuwa na uzito mkubwa katika mechi ya marudiano wiki ijayo.

Wachezaji wa Kuangaliwa

Safu ya ushambuliaji ya Simba itategemea huduma ya Kibu Denis na Jean Ahoua, ambao kila mmoja amefunga mabao matatu hadi kufika hatua hii ya fainali. Wachezaji hawa, kwa kushirikiana na Elie Mpanzu na mshambuliaji mmoja kati ya Steven Mukwala au Lionel Ateba, wanatarajiwa kuwa mwiba kwa safu ya ulinzi ya Berkane. Katika eneo la kiungo, Fabrice Ngoma na Yusuph Kagoma wataongoza vita ya kuutawala mchezo huku ngome ya ulinzi ikiongozwa na Abdulrazak Hamza, Chamou Caraboua, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ na Shomari Kapombe. Golini, Moussa Camara ataendelea kuwa chaguo la kwanza.

Uzoefu wa RS Berkane

Kwa upande wa RS Berkane, ni timu iliyo na uzoefu mkubwa katika michuano hii. Katika kipindi cha miaka sita iliyopita, wamecheza fainali nne za CAF Confederation Cup na kutwaa ubingwa mara mbili. Walipoteza fainali ya msimu uliopita dhidi ya Zamalek na msimu huu wanarejea na kiu ya kulipiza kisasi na kurejesha heshima yao.

Wakiwa na kikosi kilichojaa wachezaji wenye uwezo mkubwa, Berkane wataingia uwanjani kwa lengo moja tu—kushinda mbele ya mashabiki wao. Hii inamaanisha Simba italazimika kuwa makini katika kila idara ili kuhimili presha ya ugenini.

Hili tunabeba!

Hii ni nafasi adimu kwa Simba kuandika ukurasa mpya katika historia ya soka la Tanzania. Kwa kikosi kilicho imara na morali iliyopanda, Simba inahitaji nidhamu, umakini na ari ya ushindi ili kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kutwaa taji hilo katika mchezo wa marudiano jijini Dar es Salaam/Zanzibar.

Ingawa RS Berkane ni timu ya kuogopwa, Simba wana kila sababu ya kuamini kuwa huu ni wakati wa kung’ara na kuionyesha Afrika kuwa sasa wamefika katika daraja la juu la ushindani.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.