Yanga mikononi mwa JKT Tanzania, nusu fainali CRDB Cup

Joel JJ By Joel JJ • 18th May 2025


Yanga mikononi mwa JKT Tanzania, nusu fainali CRDB Cup

Leo Jumapili, Mei 18, macho na masikio ya wapenda soka nchini yatakuwa mkoani Tanga kwenye Uwanja wa Mkwakwani, ambako mabingwa watetezi Yanga SC watavaana na JKT Tanzania katika nusu fainali ya kwanza ya Kombe la CRDB.

Huu utakuwa ni mchezo wa tatu kwa timu hizi kukutana msimu huu. Yanga ilishinda mchezo wa kwanza wa Ligi Kuu ya NBC kwa mabao 2-0 kabla ya JKT Tanzania kuonyesha ubora wao na kuilazimisha Yanga sare tasa katika mchezo wa marudiano.

Kwa mantiki hiyo, pambano hili linatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa huku kila upande ukijivunia sababu za msingi kutaka kushinda.

Wananchi Watafuta Historia

Yanga SC wanasaka nafasi ya kutinga fainali ya Kombe la CRDB kwa mara ya tano mfululizo, wakitafuta kulinda heshima yao kama mabingwa watetezi wa taji hilo kwa misimu mitatu mfululizo.

Ushindi leo si tu utaendeleza rekodi yao nzuri, bali pia utawaweka katika nafasi ya kutetea taji lao kwa msimu wa nne mfululizo — jambo ambalo litakuwa la kihistoria katika soka la Tanzania.

Kocha Mkuu wa Yanga, Miloud Hamdi, akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jana, alithibitisha kuwa atashusha kikosi chake bora zaidi kuhakikisha anapata matokeo mazuri.

"Tunajua umuhimu wa mchezo huu, hatutaki kupoteza nafasi. Tutatumia wachezaji wetu muhimu kwa ajili ya kuhakikisha tunashinda na kufuzu fainali," alisema Hamdi.

JKT Tanzania wapambana kutengeneza Historia

Kwa upande wa JKT Tanzania, huu ni mchezo wao wa kwanza kabisa kufika hatua ya nusu fainali katika historia ya michuano hii. Hii ni nafasi ya dhahabu kwao kuandika historia mpya na kutinga fainali ya kwanza, huku ndoto ya kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika (CAF CC) ikiwapeleka vitani 

Motisha kwa kikosi cha JKT Tanzania ni kubwa. Wameonyesha uimara wao msimu huu na wataingia dimbani kuwapa upinzani Yanga na pengine kuwashtua mabingwa hao watetezi.

Ratiba ya Mchezo

Mchezo huu wa kusisimua utapigwa saa 9:30 Alasiri kwenye uwanja wa Mkwakwani. Endapo dakika 90 za kawaida zitamalizika kwa sare, kutakuwa na dakika 30 za nyongeza, na iwapo bado mshindi hatapatikana, changamoto ya mikwaju ya penalti itaamua nani atatinga fainali.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.