Aziz Ki atimkia Wydad Athletic

Joel JJ By Joel JJ β€’ 19th May 2025


Aziz Ki atimkia Wydad Athletic

Jana ilikuwa siku ya hisia kali kwa mashabiki wa Yanga SC – si tu kwa sababu ya ushindi mzuri wa mabao 2-0 dhidi ya JKT Tanzania katika nusu fainali ya Kombe la CRDB, bali pia kwa heshima ya kipekee iliyotolewa kwa kiungo mshambuliaji Stephane Aziz Ki.

Kupitia kitambaa cha unahodha alichovishwa, mashabiki na timu walionesha wazi kuwa huenda huu ukawa ulikuwa mchezo wake wa mwisho ndani ya jezi ya Yanga.

Aziz Ki, ambaye ni mfungaji bora na mchezaji bora wa Ligi Kuu ya NBC msimu uliopita, anatarajiwa kujiunga na miamba wa soka kutoka Morocco, Wydad Athletic Club.

Taarifa za makubaliano kati ya Yanga na Wydad zilikuwepo kwa muda mrefu, zikisubiri tu hitimisho la msimu ili kuhalalisha safari ya kiungo huyo kwenda katika hatua nyingine ya mafanikio ya soka lake.

Kwa bahati mbaya, kuchelewa kumalizika kwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara kumepelekea kuharakishwa kwa safari ya Aziz Ki, kwani Wydad wanajiandaa kwa michuano ya Kombe la Dunia la Klabu linalotarajiwa kufanyika Marekani kuanzia Juni 15.

Hii ina maana kuwa mechi zilizobakia za Ligi Kuu Aziz Ki hatakuwa sehemu ya kikosi cha Yanga

Katika misimu yake mitatu akiwa na Yanga, Aziz Ki ameacha alama isiyofutika: amekuwa kiungo wa ubunifu, mshambuliaji wa kuaminika, na kiongozi wa kipekee. Ametwaa makombe, ametengeneza mabao, na zaidi ya yote – amekuwa sehemu ya mafanikio ya Yanga


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.