Singida Black Stars yaipania Simba

Joel JJ By Joel JJ β€’ 26th May 2025


Singida Black Stars yaipania Simba

Kocha wa Singida Black Stars raia wa Kenya, David Ouma amesema mechi ya kirafiki dhidi ya Yanga imewapa morali wachezaji wakati huu wakijiandaa kucheza na Simba katika mechi mbili za Ligi Kuu Bara na Kombe la Shirikisho (FA).

Katika mechi hiyo iliyopigwa Alhamisi iliyopita kwenye Uwanja wa KMC Complex uliopo Mwenge, Dar es Salaam, Singida ilishinda kwa mabao 3-2 yaliyofungwa na Elvis Rupia, Jonathan Sowah na Arthur Bada, huku yale ya Yanga yakifungwa na Prince Dube na Denis Nkane.

Ouma amesema kwa sasa wachezaji wote wako katika hali nzuri na utimamu wa kimwili, na wapo tayari kucheza na Simba katika mechi hizo muhimu zijazo, licha ya kukiri ugumu uliopo kutokana na ubora wa wapinzani wao.

"Tunakwenda kucheza mechi mbili mfululizo na Simba ambazo kwetu tunazichukua kwa umuhimu mkubwa sana. Malengo yetu makubwa yalikuwa ni kupata tiketi ya CAF ambayo tayari tumefanikiwa sasa kilichobaki ni kuendeleza heshima yetu," alisema.

Kocha huyo alisema licha ya ugumu wa mechi hiyo, lakini watapambana kuonyesha ushindani mkubwa wakianzia na ya Ligi Kuu Mei 28 kwenye Uwanja wa KMC Complex kisha na ile ya nusu fainali ya Kombe la FA itakayopigwa Mei 31.

Timu hiyo imepata tiketi ya kushiriki michuano ya CAF msimu ujao baada ya Yanga kuifunga JKT Tanzania kwa mabao 2-0 katika mechi ya nusu fainali ya Kombe la FA, hivyo kujihakikishia kumaliza nafasi ya tatu au ya nne msimu huu.

Mwanaspoti


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.