Dakika 180 za Simba mbele ya Singida BS

Joel JJ By Joel JJ β€’ 28th May 2025


Dakika 180 za Simba mbele ya Singida BS

Leo Jumatano, Mei 28, 2025, klabu ya Simba SC itashuka dimbani katika uwanja wa KMC Complex kuikabili Singida Black Stars kwenye mchezo wa ligi kuu ya NBC – mechi ya kiporo ambayo huenda ikaamua mwelekeo wa Simba katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.

Mchezo huu ni muhimu kwa Simba kushinda ili kusalia katika mbio za ubingwa wa ligi kuu msimu huu kabla ya mchezo dhidi ya Yanga SC uliopangwa kuchezwa Juni 15, 2025.

Baada ya mechi hii ya leo, Simba na Singida Black Stars watakutana tena siku tatu zijazo, Mei 31, 2025, katika nusu fainali ya Kombe la FA kwenye Uwanja wa Tanzanite Kwaraa, mjini Babati.

Hizi ni siku tatu zinazoweza kutafsiri hatima ya Simba msimu huu. Ushindi dhidi ya Singida leo unaweza kuwa chachu ya matumaini kwa Simba kuelekea mchezo mwingine mgumu wa nusu fainali ya Kombe la CRDB.

Unaweza kusema mechi hizi mbili dhidi ya Singida BS zinabeba matumaini ya Simba kushinda mataji makubwa yaliyobaki baada ya kulipoteza kombe la Shirikisho (CAF CC) lililochukuliwa na RS Berkane Jumapili iliyopita

Watani zao Yanga tayari wameshatinga fainali ya Kombe la CRDB baada ya kuifunga JKT Tanzania kwa mabao 2-0, na wanaongoza msimamo wa Ligi Kuu Bara, hii imeongeza presha kubwa kwa Simba kuhakikisha hawapotezi pointi leo.

Kwa Singida Black Stars, presha ni ndogo kwani tayari wamejihakikishia nafasi ya kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika msimu ujao. Hata hivyo, watatumia mechi hizi kama fursa ya kuonyesha ubora wao na kujiimarisha zaidi kabla ya kampeni za kimataifa.

Macho yote yatakuwa KMC Complex na kisha kuelekea Babati – katika mechi muhimu kwa Simba kuhakikisha inakuwa na nafasi ya kushinda mataji msimu huu


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.