Afisa Habari wa Bodi ya Ligi (TPLB) Karim Boimanda amesema maandalizi kuelekea mchezo wa ligi kuu namba 184 kati ya Yanga dhidi ya Simba uliopangwa kupigwa Juni 15 katika uwanja wa Benjamin Mkapa yanaendelea vizuri
Boimanda amesema wadau wote wanaohusika na mchezo huo wanaendele na maandalizi huku Bodi ikihakikisha taratibu zote za msingi ili kufanikisha mchezo huo zinakamilika
Licha ya kauli za kutocheza mchezo huo zinazotoka upande wa Yanga, Boimanda amesema kama mwenyeji Yanga inawajibika kwa upande wake lakini bodi nayo itawajibika kwa upande wake pale wakati utakapowadia
Aidha kuhusu kutotangazwa kwa viingilio vya mchezo huo mpaka sasa, Boimanda amesema utaratibu wa viingilio ni uleule kwani viingilio vilivyotumika katika mchezo uliopaswa kupigwa March 08 ni vilevile kwa maana wale ambao walikata tiketi wakati ule watazitumia
"Maandalizi ya michezo mikubwa kama hii yako katika hatua mbalimbali, kwa sasa bado hatujafikia hatua ya kutaka kupata ripoti kutoka kwa timu mwenyeji ambaye anahusika kwa asilimia kubwa katika maandalizi likiwemo suala la viingilio"
"Kitu ambacho wadau wanapaswa kukumbuka ni kuwa mchezo huu ulishajadiliwa kuhusiana na viingilio vyake na tiketi zilianza kuuzwa na mpaka sasa ninapozungumza kuna tiketi zilinunuliwa na bado zipo kwenye kadi za mashabiki wetu wa zamani ambao walizinunua na tulishaeleza mara kadhaa tiketi zile hazijapotea zitatumika katika mchezo huu"
"Hakuna mjadala mkubwa kwenye suala la tiketi kwa sasa tunasubiri ufike wakati wa kutangaza kuendelea kuuza tiketi ambazo zilisitishwa baada ya mchezo ule kuahiridhwa"
"Tunaamini timu mwenyeji anaendelea na maandalizi yake kwa kuwa bado haujafikia wakati wa sisi kutaka kufahamu wamefikia wapi katika maandalizi hayo. Wakati utakapofika tutakuwa na vikao vyetu kupeana taarifa kuhusu maandalizi yote kwa ujumla," alisema Boimanda
Wakati taratibu za mchezo huo zikiendelea, viongozi wa Yanga wameendelea kushikilia msimamo kuwa Juni 15 hawatapeleka timu uwanjani



