Simba yafunguka tetesi za kumsajili Fei Toto

Joel JJ By Joel JJ • 11th June 2025


Simba yafunguka tetesi za kumsajili Fei Toto

Katika kipindi ambacho tetesi za usajili zinaendelea kushika kasi, jina la kiungo mahiri wa Azam FC, Feisal Salum ‘Fei Toto’, limekuwa likitajwa sana kuhusishwa na klabu ya Simba SC.

Hata hivyo, klabu hiyo kupitia kwa Meneja wa Habari na Mawasiliano, Ahmed Ali, imeweka mambo sawa – kwa sasa, ni kimya na heshima kwa mkataba wa mchezaji huyo.

Ahmed Ali amesema wazi kuwa Feisal ni mchezaji wa kiwango cha juu ambaye timu yoyote ya Tanzania ingetamani kuwa naye, lakini Simba haiwezi kuingia kwenye mjadala wa usajili wake kwa sasa kwa sababu bado ana mkataba na Azam FC.

Feisal ni mchezaji mzuri ambaye kila timu hapa nchini inatamani kuwa naye. Lakini kwa sasa ni mchezaji wa Azam FC, lazima tuheshimu hilo. Tunafahamu ni makosa kuzungumzia mchezaji wa timu nyingine,” alisema Ahmed.

Akaongeza kuwa Simba, ikiwa itamhitaji, itafuata taratibu zote za kisheria na kiuanamichezo

Mashabiki wetu wanatamani kumuona Feisal akiichezea timu yetu, hivyo hilo litabaki kama matamanio tu kwa sasa,” alihitimisha.

Fei Toto amekuwa miongoni mwa wachezaji walioibeba Azam FC msimu huu, akiongoza ligi kuu ya NBC kwa asisti 13, rekodi ambayo imewavutia vigogo wa soka la Tanzania. Uchezaji wake wenye akili ya ziada, pasi zenye macho na kasi ya kupenya safu ya ulinzi umemfanya kuwa lulu ya kiungo cha ushambuliaji.

Kwa muda sasa, uvumi umeenea kuwa Simba wanataka kuongeza nguvu kwenye safu ya kiungo kwa kumleta Feisal Msimbazi, wakiamini atatoa chachu mpya kwenye mashambulizi yao, hususan katika michuano ya kimataifa inayowasubiri msimu ujao.

Pamoja na Simba kujizuia kuzungumzia suala hilo moja kwa moja, wachambuzi wa soka wanasema kauli ya Ahmed Ali ni dalili ya uwezekano wa dili hilo kuwepo mezani, likisubiri muda muafaka.

Kwa sasa, mashabiki wa Simba na hata wale wa Azam wameshikilia pumzi wakisubiri dirisha la usajili kufunguliwa rasmi, ambapo ukweli utawekwa wazi


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.