Ukimya umeendelea kutawala katika kambi ya klabu ya Simba kuelekea mechi za kuhitimisha msimu wa 2024/2025 wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Licha ya kuonekana kutii maamuzi ya mamlaka, ni wazi uongozi wa Wekundu wa Msimbazi haujaridhishwa na mchakato wa kusogeza mbele mechi yao dhidi ya Yanga mechi ya Kariakoo Dabi ambayo sasa itapigwa Juni 25 badala ya Juni 15
Tofauti na ilivyozoeleka kwa Simba, hakuna taarifa za maandalizi ya timu kuelekea mechi hizo na zaidi kurasa za mitandao ya kijamii za klabu ni kama nazo zimepewa likizo kwani tangu yatangazwe maamuzi ya kusogeza mchezo namba 184 mbele, sio zaidi ya machapisho manne yaliyowekwa.
Baada ya kupata mapumziko ya siku mbili, kikosi cha Simba kilirejea mazoezini kimya kimya, wakijiandaa kwa mchezo unaofuata dhidi ya KenGold FC utakaopigwa Juni 18 kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, Tabora. Simba imeondoka Dar es Salaam mapema Jumanne kuelekea Tabora tayari kwa mchezo huo
KenGold, waliokwisha shuka daraja, nao wamechelewa kuwasili Tabora kwa maandalizi ya mechi hiyo. Hadi kufikia juzi, taarifa kutoka ndani ya timu hiyo zilidai wachezaji walikuwa wakisubiri kupewa nauli kila mmoja akiwa nyumbani kwao. Imeelezwa kuwa walitarajiwa kuanza kuwasili Tabora jana Jumatatu, ikiwa ni siku mbili tu kabla ya mechi.
Je, ukimya wa Simba unamaanisha nini?
Baadhi ya wachambuzi wa soka wanadai ukimya wa Simba ni mkakati. Ni njia ya kuondoa presha kwa wachezaji na kujiandaa kwa tahadhari, wakilenga mechi ya Dabi ambayo inaweza kuamua ubingwa.
Wengine wanaona huu ni ukimya wa huzuni, kuonyesha kutofurahishwa na maamuzi ya Bodi ya ligi kusogeza mbele mchezo namba 184



