Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN 2025) inakaribia kwa kasi, huku maandalizi yakifikia kilele katika nchi tatu zinazoshirikiana kuandaa tukio hili kubwa la soka Tanzania, Kenya, na Uganda.
Kwa mara ya kwanza katika historia ya CHAN, michuano hii itachezwa katika mfumo wa ushirikiano wa kikanda, hali inayoongeza upekee na uzito wa mashindano haya.
Ufunguzi wa Kihistoria – Agosti 2, Benjamin Mkapa
Tarehe 2 Agosti 2025, macho ya Afrika yote yataelekezwa jijini Dar es Salaam, ambapo sherehe ya uzinduzi wa CHAN 2025 itafanyika katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, moja ya viwanja bora kabisa barani Afrika.
Baada ya sherehe hizo, mchezo wa ufunguzi utapigwa uwanjani hapo, ukiashiria mwanzo rasmi wa safari ya kuelekea ubingwa wa Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani.
Fainali Nairobi, Mechi ya Tatu Kampala
Michuano ya mwaka huu inazidi kuwa ya kipekee kwa sababu fainali itachezwa nchini Kenya katika Uwanja wa Kimataifa wa Kasarani, Nairobi, mnamo Agosti 30, 2025.
Wakati huo huo, mashabiki wa Uganda pia hawajachwa nyuma, kwani mechi ya kutafuta mshindi wa tatu itafanyika jijini Kampala. Uamuzi huu wa kugawanya mechi muhimu katika nchi tatu za Afrika Mashariki unaashiria umoja, ushirikiano na dhamira ya pamoja ya kukuza soka la Afrika Mashariki
Makundi ya Michuano – Tanzania na Zanzibar Mwenyeji wa Mechi za Makundi
Kundi B: Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam
Tanzania
Madagascar
Afrika ya Kati
Burkina Faso
Mauritania
Mashabiki wa Tanzania watafurahia kuwaona Taifa Stars wakicheza nyumbani katika uwanja wao wa nyumbani, wakipambana dhidi ya mataifa yenye uzoefu mkubwa katika soka la ndani.
Kundi D: New Amaan Stadium, Zanzibar
Senegal
Congo Brazzaville
Sudan
Nigeria
Kwa upande wa Zanzibar, New Amaan Stadium utakuwa jukwaa la Kundi D, likiwahusisha vigogo wa soka kama Nigeria na Senegal. Hii ni fursa adimu kwa visiwa hivyo kuandaa mechi za kiwango cha juu na kuongeza thamani ya soka la Zanzibar.



