Klabu ya Simba SC iko katika hatua za mwisho za mazungumzo na Kocha Mkuu wao, Fadlu Davids, kuhusu kuhuisha mkataba wake ambao umemalizika rasmi.
Taarifa kutoka ndani ya klabu hiyo zimeeleza kuwa tayari Fadlu amekutana na viongozi wa juu wa Simba SC kukamilisha mazungumzo kwa ajili ya kuongeza muda wa mkataba wake.
Hatua hii imechochewa na kazi nzuri aliyoifanya msimu huu, ambapo Simba imeonyesha kiwango bora uwanjani licha ya kuwa hakufanikiwa kushinda taji lolote.
Rais wa heshima wa klabu hiyo, Bilionea Mohammed Dewji ‘Mo’, ameripotiwa kumhakikishia Fadlu mkataba mpya, kama ishara ya kuthamini mchango wake na kuendelea na mpango wa muda mrefu wa maendeleo ya timu.
Kwa mujibu wa taarifa, Fadlu tayari amewasilisha mapendekezo yake kwa uongozi wa klabu — ikiwa ni pamoja na maboresho kadhaa kwenye upande wa kikosi. Hii ni sehemu ya masharti aliyoweka ili kuendelea na kazi Simba.
Mapendekezo hayo yanahusisha usajili mpya pamoja na kuboresha baadhi ya maeneo ya kikosi yaliyobainika kuwa na changamoto msimu uliomalizika.
Akizungumza mara baada ya mchezo dhidi ya watani wa jadi Yanga, Fadlu alisema:
“Nitawasilisha mapendekezo yangu kwa uongozi, tutaona wao wanasemaje. Kama kile wanachohitaji kiko sawa na ninachohitaji, basi tutasonga mbele,” alisema
Fadlu alijiunga na Simba kwa mkataba wa mwaka mmoja ambao sasa umefikia mwisho. Mazungumzo ya mkataba mpya yanahusisha pia benchi lake lote la ufundi alilokuja nalo, ambalo linajumuisha watu wengine kama Kocha Msaidizi, Kocha wa Viungo, pamoja na mchambuzi wa video (Video Analyst).



