Kiungo mshambuliaji kutoka Burkina Faso, Stephane Aziz Ki, ambaye alijiunga na klabu ya Wydad Casablanca mwezi uliopita akitokea Yanga SC ya Tanzania, sasa yuko njia panda baada ya kuonekana kutokuwa katika mipango ya kocha mpya wa klabu hiyo, Mohamed Benhachem.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Morocco, Benhachem hajamjumuisha Aziz Ki kwenye orodha ya wachezaji watano wa kigeni ambao atawategemea kwa msimu ujao wa Ligi Kuu ya Morocco (Botola).
Kwa mujibu wa kanuni za ligi hiyo, kila klabu inaruhusiwa kusajili wachezaji wa kigeni wasiozidi watano. Wydad tayari ina wachezaji wanane wa kigeni, hivyo baadhi yao watalazimika kuondoka au kutolewa kwa mkopo.
Aziz Ki, ambaye alitarajiwa kuwa miongoni mwa wachezaji muhimu wa Wydad katika kampeni ya kimataifa, ameonekana kutopewa nafasi kubwa na kocha Benhachem. Katika michuano ya Kombe la Dunia la Klabu, alichezeshwa kwa dakika 7 tu katika jumla ya mechi mbili, jambo linaloashiria wazi kutokuwa sehemu ya mipango ya muda mrefu ya kocha huyo.
Habari njema kwa mashabiki wa Yanga ni kuwa kuna uwezekano mkubwa wa nyota huyo kurejea Jangwani. Taarifa zinaeleza kuwa Yanga na Wydad walikubaliana masharti ya uhamisho wa Aziz Ki, lakini kuna kiasi cha fedha ambacho Wydad wanapaswa kulipa kabla ya Julai 10 ili kukamilisha rasmi uhamisho huo. Iwapo Wydad watashindwa kutimiza masharti hayo, inawezekana Ki akarudi Yanga kama sehemu ya makubaliano.
Ikumbukwe kuwa usajili wa Aziz Ki kwenda Wydad ulikuwa ni pendekezo la aliyekuwa kocha wa klabu hiyo, Rulani Mokwena, ambaye alivutiwa naye baada ya mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na Mamelodi Sundowns. Hata hivyo, Mokwena aliachana na Wydad baada ya msimu kumalizika, hali iliyopelekea mwelekeo mpya wa benchi la ufundi na mustakabali wa Ki kuwa tata.
Kwa upande mwingine, mchezaji chipukizi Mtanzania Selemani Mwalimu (19) amenusurika katika orodha ya wachezaji wanaotarajiwa kuondoka baada ya kusajiliwa kama mchezaji wa timu ya vijana, hivyo hayumo katika orodha ya wachezaji wa kigeni wa kikosi cha kwanza.
Mashabiki wa Yanga wanasubiri kwa hamu kuona hatima ya kiungo wao wa zamani ambaye aliisaidia timu yao kwa mafanikio makubwa katika misimu mitatu iliyopita. Je, Aziz Ki atarejea Jangwani? Muda utasema, lakini dalili zinaonyesha mlango wa kurudi Yanga bado uko wazi.