Klabu ya Simba SC imefanikiwa kufikia makubaliano ya kuongeza mkataba wa mwaka mmoja na Kocha Mkuu wao, Fadlu Davids, pamoja na benchi lake lote la ufundi. Hii ni baada ya mazungumzo yaliyofanyika kati ya Fadlu na Rais wa heshima wa klabu hiyo, Mohammed Dewji 'Mo', kukamilika kwa mafanikio mwishoni mwa msimu uliopita.
Fadlu, ambaye alijiunga na Simba msimu uliopita akiwa na timu yake ya karibu ya wataalamu akiwemo kocha msaidizi, kocha wa viungo na mtaalamu wa kuchambua video, alisaidia Simba kuimarika kimchezo na kufikia mafanikio muhimu, ikiwemo kumaliza Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara katika nafasi ya pili kwa pointi 78 na kufika fainali ya Kombe la Shirikisho la CAF dhidi ya RS Berkane ya Morocco.
Mkataba wao wa awali ulikuwa wa msimu mmoja na ulimalizika mwishoni mwa msimu. Hata hivyo, kutokana na mwenendo chanya wa timu na mipango ya muda mrefu ya maendeleo, Bodi ya Wakurugenzi ya Simba iliyokutana juzi jijini Dar es Salaam ilipitisha rasmi mpango wa kuongeza mkataba wa Fadlu na benchi lake kwa mwaka mwingine. Mkataba huo mpya pia una kipengele kinachoruhusu kuongezwa kwa mwaka mmoja zaidi kutegemeana na mafanikio.
Kwa sasa, benchi la ufundi linatarajiwa kurejea kutoka mapumziko mafupi na kuanza rasmi maandalizi ya msimu mpya. Fadlu tayari amewasilisha ripoti kamili ya tathmini ya msimu uliopita, ikiwa na mapendekezo ya usajili wa wachezaji wapya wenye ubora wa kimataifa, uzoefu wa mashindano makubwa, pamoja na uwezo wa kutekeleza maagizo ya kiufundi kwa ufasaha.
Aidha, kocha huyo amependekeza kufanyika kwa uchunguzi wa kina wa kikosi kilichopo kwa sasa, akisisitiza kuwa ni wachezaji watakaokidhi vigezo vya ubora na nidhamu ya kiufundi tu watakaosalia.