Mabosi wa Simba wako sokoni kutafuta golikipa mwingine wa Kimataifa na endapo kama wafanikiwa katika mpango wake, ni wazi golikipa wake namba moja Moussa Camara hatma yake itakuwa shakani
Kuanzia msimu ujao mabadiliko ya kanuni hayataruhusu klabu kuwa na zaidi ya golikipa mmoja wa kigeni
Licha ya kuibuka na tuzo ya golikipa bora wa ligi kuu ya NBC msimu uliomalizika baada ya kukusanya cleanshet 19 akiifikia rekodi iliyowahi kuekwa na Aishi Manula msimu wa 2017/18, Camara anaweza kuponzwa na makosa aliyofanya kwenye mechi chache ambazo kama Simba ingepata matokeo mazuri, basi leo hadithi zingekuwa tofauti
Camara ambaye alitua Simba mwanzoni mwa 2024-2025 akitokea Horoya ya Guinea, amekuwa kipa namba moja kikosini baada ya Ayoub Lakred kuwa na majeraha ya muda mrefu na kuondolewa kwenye usajili wa msimu uliopita
Licha ya kuonyesha kiwango bora, lakini kuna makosa aliyofanya katika baadhi ya mechi za ligi na hata mechi za Kimataifa
Camara alicheza mechi zote za kimataifa za Simba ikicheza fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika na kupoteza mbele ya RS Berkane ya Morocco.
Katika ligi Camara amecheza mechi 28 kwa dakika 2,520 kati ya mechi 30, ndiye ameibuka kinara wa clean sheet akimaliza na 19, huku akiruhusu mabao 13.
Miongoni mwa makosa aliyofanya yaliyoigharimu Simba ni mechi mbili za ligi dhidi ya Yanga Oktoba 19, 2024 mpira wa faulo uliopigwa na Clatous Chama dakika ya 86 ukionekana kwenda nje aliufuata na kujikuta anaurudisha ndani Maxi Nzengeli akaupiga haraka Kelvin Kijili akajifunga, likawa bao pekee lililoipa Yanga ushindi wa 1-0.
Pia Juni 25, 2025 alitoka golini na kwenda kumfanyia faulo Pacome Zouzoua Simba ikaruhusu bao la kwanza na kupoteza kwa mabao 2-0.
Kabla ya hapo, katika sare ya 2-2 dhidi ya Coastal Union, Oktoba 4, 2024 alifanya makosa mawili yaliyozaa mabao wakati Simba ikiwa mbele kwa 2-0 na mwisho mchezo ukaisha sare ya 2-2.
Baada ya kikao cha Bodi kilichofanyika jijini Dar es salaam hivi karibuni, Simba imeidhinisha kusaka mlinda lango mwingine mwenye sifa na vigezo vilivyoidhinishwa na benchi la ufundi, lakini kama hawatampata basi Camara atanusurika
Lakini ni wazi Camara atahitaji kufanyia kazi baadhi ya mapungufu yaliyoonekana ili kuhakikisha anaipa uhakika Simba katika malengo ya kuwania mataji



