Mashabiki wa Simba SC wamejaa hamasa. Kwa miezi kadhaa sasa, uvumi umeenea kwamba kiungo nyota wa Azam FC, Feisal Salum, yupo mbioni kujiunga na mabingwa hao wa zamani wa Tanzania katika dirisha hili la usajili la Julai na dili linaonekana kuwa karibu kutimia.
Feisal ni mchezaji mwenye kipaji cha hali ya juu, kwa sasa anatizamwa kama kiungo bora katika eneo la ushambuliaji msimu uliomalizika akiwa kinara wa kutoa pasi za mabao (13) wakati msimu mmoja nyuma alipachika mabao 19 na pasi nane za mabao
Simba wamehusishwa na Fei Toto tangu mwishoni mwa mwaka 2024, taarifa kutoka ndani ya uongozi imethibitisha Wekundu hao wa Msimbazi tayari wana makubaliano binafsi na Fei Toto kilichobaki ni utaratibu wa kumalizana na Azam Fc
Fei Toto bado ana mkataba wa mwaka mmoja na Azam Fc ambao utamalizika Juni 2026. Kuna taarifa kuwa Azam Fc wana makubaliano na klabu yake ya zamani Yanga kuwa endapo Azam Fc itamuuza ndani ya nchi itapaswa kulipa Tsh Bilioni 1 kwa Yanga
Licha ya Kaizer Chiefs kuwasilisha ofa kwa Azam Fc kutaka kumnunua, fundi huyo kutoka Zanzibar ameweka ngumu akisubiri uhamisho wake kuelekea Msimbazi ukamilike
Ni usajili unaosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa Simba SC hasa ikizingatiwa timu yao inasukwa upya kwa ajili ya msimu ujao wa mafanikio baada ya kwenda misimu minne bila kushinda mataji makubwa
Kwa sasa mitandaoni mashabiki wa Simba wanawasukuma viongozi wao kuharakisha kukamilisha usajili huo kwani zipo taarifa waajiri wake wa zamani Yanga wanamshawishi arejee katika klabu hiyo licha ya mvutano uliojitokeza baina yao wakati Feisal anataka kujiunga na Azam Fc
Katika moja ya mahojiano yake, Mfadhili wa zamani wa Simba Azim Dewji ambaye ni baba mdogo wa mwekezaji wa Simba Bilionea Mohammed Dewji 'Mo', alidokeza kuwa Fei Toto msimu ujao atacheza Simba
"Kuna mambo fulani fulani yanawekwa sawa lakini naamini kila kitu kitakamilika na Fei atacheza Simba msimu ujao," alisema