Dodoma Jiji kumshusha kocha Mcongo

Joel JJ By Joel JJ • 8th July 2025


Dodoma Jiji kumshusha kocha Mcongo

Mabosi wa Dodoma Jiji FC wako katika mazungumzo ya kuipata saini ya aliyekuwa kocha wa Tabora United, Mkongomani Anicet Kiazayidi baada ya kuvutiwa na uwezo wake, wakiamini atatengeneza kikosi bora kitakacholeta ushindani mkubwa msimu ujao.

Taarifa za uhakika zinaeleza kocha Mkuu wa Dodoma Jiji, Mecky Maxime aliyejiunga na timu hiyo, Juni 19, 2024, akitokea Ihefu ambayo kwa sasa ni Singida Black Stars, huenda akaachana na kikosi hicho licha ya mkataba alionao.

Chanzo kutoka ndani ya timu hiyo, kimeeleza kuwa Maxime amebakisha mkataba wa mwaka mmoja wa kuendelea kuiongoza kwa msimu ujao, ingawa huenda akaondoka kutokana na kutokuwa na maelewano mazuri na mabosi wake kwa siku za hivi karibuni.

“Amekuwa na maelewano mabaya na viongozi wa juu na yeye mwenyewe amejishtukia akiamini huenda akaondoka kutokana na hali iliyopo, hadi sasa hakuna muafaka uliofikiwa kwa sababu ana mkataba pia wa mwaka mmoja uliobaki,” kilisema chanzo hicho.

Akizungumzia juu ya taarifa hizo, Katibu Mkuu wa Dodoma Jiji, Fortunatus Johnson alisema anachotambua Maxime ana mkataba wa mwaka mmoja uliobakia, hivyo kuhusu mambo mengine ya kuondoka kwake bado hakuna kilichofanyika baina ya pande mbili.

“Tangu tumemaliza Ligi Kuu msimu huu wa 2024-2025, Juni 25, 2025, tunatarajia kufanya kikao chetu Julai 10, kwa ajili ya kujadili mambo mbalimbali ya kuboresha timu yetu, hivyo hayo ndiyo ninaweza kuyazungumzia kwa sasa,” alisema Fortunatus.

Hata hivyo, licha ya kauli ya Fortunatus, Dodoma wamefanya mazungumzo na Anicet kwa ajili ya kuifundisha msimu ujao, baada ya kuonyesha uwezo mkubwa msimu uliopita alipokuwa anaifundisha Tabora United.

Anicet alijiunga na Tabora Novemba 2, 2024, ili kuchukua nafasi ya Mkenya Francis Kimanzi aliyeondoka Oktoba 21, 2024, ingawa Mkongomani huyo aliondoka Machi 28, 2025, baada ya kufikia makubaliano ya kusitisha mkataba wake wa pande mbili.

Mwanaspoti


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.