Kocha Mpya wa Yanga ni huyu

Joel JJ By Joel JJ • 16th July 2025


Kocha Mpya wa Yanga ni huyu

Baada ya tetesi zilizoenea kwa wiki kadhaa, hatimaye ukweli umefahamika, aliyekuwa kocha msaidizi wa Mamelodi Sundowns, Romain Folz, yupo mbioni kutangazwa rasmi kama kocha mkuu mpya wa klabu ya Yanga.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 35 anarudi katika soka la CAF Champions League kupitia dili hili kubwa na vigogo hao wa soka Afrika Mashariki waliomaliza msimu wa 2024/25 wakiwa na mataji yote ya ndani.

Inaelezwa kuwa Rais wa klabu ya Yanga, Injinia Hersi Ally Said, alipata mapendekezo ya nguvu ya kumuajiri kocha huyo raia wa Ufaransa kutoka kwa Arsène Wenger, Mkuu wa Maendeleo ya Soka Duniani ndani ya FIFA walipokutana kwenye Kombe la Dunia la Klabu hivi karibuni.

Vyanzo vya ndani ya klabu vimebainisha kuwa Folz tayari yuko nchini na huenda akatambulishwa wiki ijayo kuchukua rasmi nafasi ya Miloud Hamdi aliyejiunga na klabu ya Ismaily ya Ligi Kuu ya Misri.

Folz anakuja Yanga akiwa na historia ya aina yake akizitumikia klabu mbalimbali na hata timu za Taifa katika majukumu ya Kocha Mkuu, Kocha Msaidizi au Mkurugenzi wa ufundi

Alimaliza msimu uliopita akiwa na Olympique Akbou ya Algeria ambapo aliisaidia klabu hiyo kubaki ligi kuu katika mechi nane za mwisho. Pia amewahi kupitia klabu kama Township Rollers, Marumo Gallants, AmaZulu na Horoya AC.

Kwa kujiunga na Yanga, Folz anafungua ukurasa mpya katika safari yake ya ukufunzi, safari inayotarajiwa kuwa ya changamoto lakini yenye matarajio makubwa, hasa katika kuhakikisha Yanga SC inasalia kuwa nguvu ya kutisha kwenye soka la Afrika.


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.