Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa klabu ya Azam FC, Thabit Zacharia maarufu kama Zakazakazi, amefunguka kuhusu sababu zinazowazuia kumuuza kiungo mshambuliaji Feisal Salum Fei Toto kwa klabu ya Simba SC.
Kupitia mahojiano aliyofanya na redio moja maarufu jijini Dar es salaam, Zakazakazi alisema wazi kuwa Azam FC haiwezi kumuuza mchezaji huyo kwa Simba kutokana na kipengele maalum kilichopo kwenye mkataba wao na klabu ya Yanga, walipomnunua mchezaji huyo awali.
"Hatuwezi kumuuza Feisal kwenda Simba kwa sababu sidhani kama Simba wana pesa za kuweza kumnunua Feisal," amesema.
Zakazakazi ameweka wazi kuwa wakati Azam FC ilipomsajili Feisal kutoka Yanga SC, walikubaliana kuwa endapo mchezaji huyo atauzwa kwa Simba, basi Azam italazimika kuilipa Yanga fidia ya shilingi bilioni moja za Kitanzania.
"Wakati tunamchukua Feisal kutoka Yanga, yapo makubaliano ya kimkataba kuwa endapo tutamuuza mchezaji huyo kwa klabu ya Simba, tunapaswa kuilipa Yanga Tsh Bilioni 1," alifichua.
Ameongeza kuwa ili kufanikisha uhamisho huo, Simba italazimika kutoa dau kubwa litakalowezesha Azam kupata faida zaidi ya fidia hiyo, jambo ambalo linaonekana kuwa gumu.
"Sasa Simba watalipa shilingi ngapi tufanye biashara? Sisi hatuko tayari kulipa Bilioni 1 kwa Yanga kama dau lao litakuwa dogo, na pia lazima walipe dau ambalo litatufanya tupate zaidi ya Yanga," alisisitiza.
Pamoja na mijadala mingi inayoendelea mitandaoni kuhusu tetesi za uhamisho wa Fei Toto kwenda Simba, Zakazakazi amesema hadi sasa hawajapokea ofa yoyote rasmi kutoka kwa Simba.