Kocha Mkuu wa Simba Fadu Davids amesema wamepokea droo ya hatua ya awali michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika na sasa wanafanya maandalizi kabambe ili kuhakikisha wanafuzu hatua ya makundi ya michuano hiyo mikubwa zaidi barani Afrika katika ngazi ya klabu
Droo ya mechi za hatua ya awali na raundi ya kwanza ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika (CAF CL) ilifanyika juzi jijini Dar es salaam ambapo Simba ilipangwa kuchuana na Gaborone United ya Botswana katika hatua ya awali
Mchezo wa kwanza utapigwa Botwana na mechi ya marudiano kupigwa wiki moja baadae jijini Dar es salaam
Aidha kama Simba itafanikiwa kutinga raundi ya kwanza, itachuana na mshindi wa mchezo kati ya Simba Bhora ya Zimbabwe dhidi ya Nsingizini Hotspurs ya Malawi
Fadlu amesema Gaborone United sio timu nyepesi lakini anafurahi kwa kuwa kikosi chake kitacheza mechi ya kwanza Botswana na kumaliza mechi ya pili uwanja wa Benjamin Mkapa
"Tunajua ligi ya mabingwa ni mashindano makubwa zaidi kuliko kombe la Shirikisho tulilocheza msimu uliopita ambalo tulianza hatua ya awali dhidi ya timu ngumu ya Al Ahly Tripoli, wakati huu tunaanza na Gaborone United"
"Tunajua haitakuwa mechi nyepesi, najua ni timu yenye wachezaji wapambanaji na wagumu wanapocheza katika uwanja wao wa nyumbani"
"Lakini sisi tunaamini katika uwezo wetu, msimu huu tumeunda timu imara zaidi ambayo inaweza kupambana katika mazingira magumu, pia tuna uzoefu baada ya ushiriki wetu michuano ya kombe la Shirikisho msimu uliopita"
"Timu yetu imeimarika zaidi na niseme tu, tuko tayari kwa michuano hii ya ligi ya mabingwa msimu huu"
"Tutafanya tathmini ya kina kabla ya kukabiliana nao, tayari tunawafahamu Jwaneng Galaxy, Township Rollers na hata hawa Gaborone United ni timu zenye uzoefu na mashindano haya"
"Tutapambana ili kuhakikisha tunavuka raundi hii," alisema Fadlu



