Kocha Mkuu wa Yanga Romain Folz jana katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Rayon Sports uliopigwa uwanja wa Amahoro huko Rwanda, aliwaanzisha wachezaji wanne wapya
Viungo Moussa Balla Conte, Mohamed Doumbia winga Celestin Ecua na mshambuliaji Andy Boyeli walianza kipindi cha kwanza katika mchezo huo ambao Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 3-1
Ukiwa ni mchezo wa kwanza wa ushindani tangu Yanga ilipoanza kujifua siku 10 zilizopita, nyota hao walionyesha umahiri wao na kuwapa matumaini mashabiki wa Yanga juu ya ubora wa timu yao siku za usoni
Conte alishirikiana vyema na safu ya ulinzi kwa kukata umeme huku Doumbia akionekana kila mahali eneo la kiungo akiichezesha timu



Ecua alionyesha hatari yake ndani ya eneo la hatari, kulikuwa na matukio ya winga huyo aliyetua kutoka Asec kufanyiwa madhambi katika eneo la hatari lakini mwamuzi hakuchukua hatua
Dakika 45 alizotumika katika mchezo huo zilimtosha Boyeli kuonyesha Yanga haikukosea kumfuata Afrika Kusini
Boyeli alifunga bao la kusawazisha la Yanga kabla ya kutengeneza bao la pili liililofungwa na Pacome Zouzoua
Baada ya mapumziko, Folz aliwatoa nyota hao akifanya mabadiliko ya karibu kikosi kizima nyota wengine wapya Lassine Kouma, Offen Chikola na Edmund John nao wakipata nafasi


Chikola alikuwa kivutio zaidi dakika 45 za kipindi cha pili akihusika katika bao la tatu lililofungwa na nahodha Bakari Nondo Mwamnyeto
Mpira wake wa kona ulitendewa haki na Mwamnyeto aliyeujaza mpira kimiani kwa kichwa na kuihakikishia Yanga taji la kwanza katika pre-season
Akizungumza baada ya mchezo huo, Folz alisema bado timu yake haijapata muunganiko lakini anawapongeza wachezaji wake kwa kutimiza angalau kwa asilimia chache ya kile walichokiandaa
"Tumekuwa na bahati mbaya kuruhusu goli la mapema ambalo ni uzembe pia muda mwingi tuliachia mipira kizembe, bado hatujazoeana kiufundi na kimbinu, niseme wazi bado tuko mbali na kile tunachokitaka," alisema Folz